Yesaya 29

Masongano na wokovu wa Yerusalemu.

1Umekwisha kuapizwa, wewe Simba wa Mungu!

Wewe Simba wa Mungu! Wewe mji, Dawidi alimotua!

Ongezeni mwaka kwa mwaka na kula sikukuu miaka mizima!

2Kisha nitamsonga Simba wa Mungu,

kuweko kipiga kite na kuugua;

ndipo, atakapokuwa mbele yangu Simba wa Mungu wa kweli.

3Ndipo, nitakapokupigia makambi, yakuzinge,

kisha nitakujengea boma la kukusonga,

nitaisimamisha hata minara, nipate kukushinda.

4Hapo ndipo, utakaponyenyekea, useme na kulala chini,

maneno yako, utakayonitolea toka mavumbini,

yatakuwa ya kujipunguza,

sauti yako itakuwa kama ya mzimu atokaye kuzimuni,

maneno yako ya kusema uvumbini

yatakuwa ya kunong'ona tu.

5Lakini mavumo ya wale wageni waliokujia

yatakuwa kama mavumbi membamba,

kweli mavumo ya hao wakorofi

yatakuwa kama makapi yapeperushwayo;

nayo yatakuwa kwa ghafula, wagunduliwe nayo.

6Maana utakaguliwa na Bwana Mwenye vikosi,

atakapokujia na kuitetemesha nchi kwa ngurumo,

kwani ni mwenye sauti kuu,

ataleta nao upepo wa kimbunga ulio wenye nguvu

na ndimi za moto ulao.

7Yatakuwa kama ndoto, mtu aliyoiota usiku,

hayo mavumo ya wamizimu waliokuja

kumshambulia Simba wa Mungu

nao waliolipigia boma lake vita na kumsonga.

8Itakuwa kama mwenye njaa anayeota akila chakula,

lakini anapoamka hakuna kitu kwake,

au kama mwenye kiu anayeota akinywa,

lakini anapoamka hutweta na kuivuta roho yake.

Hivyo ndivyo, yatakavyokuwa mavumo ya wamizimu wote,

waliokuja kuushambulia mlima wa Sioni!

Watu hawatambui maana.

9Tumbueni macho na kuyakodoa! Yatieni giza na kupofuka!

Wamelewa, lakini si kwa mvinyo,

wanapepesuka, lakini si kwa kileo.

10Kwani Bwana amewamwagia ninyi roho ya usingizi mwingi,

akayafumba macho yenu, ninyi wafumbuaji,

akavifunika vichwa vyenu, ninyi wachunguzaji.

11Hayo yote mliyoyaona yakawa kwenu kama maneno ya kitabu

kulichofungwa na kutiwa muhuri;

kama ajuaye kusoma anapewa na kuambiwa: Kisome hiki!

atajibu: Siwezi, kwani kimefungwa na kutiwa muhuri.

12Kama asiyejua kusoma anapewa na kuambiwa: Kisome hiki!

atajibu: Sijui kusoma.

13Bwana akasema:

Ukoo huu hunikaribia na vinywa vyao,

huniheshimu kwa midomo tu,

lakini mioyo yao inanikalia mbali;

kwa sababu hii hunicha bure,

kwani hufundisha mafundisho yaliyo maagizo ya watu tu.

14Kwa hiyo na mwone, ninavyoendelea

kuufanyizia ukoo huu mambo ya mataajabu na ya vioja,

werevu wao walio werevu wa kweli kwao upotee,

nao utambuzi wa watambuzi wao usionekane.

15Yatawapata wao walao njama,

kwamba: wamfiche Bwana mashauri yao!

Nao wafanyao gizani kazi zao na kusema:

Yuko nani anayetuona? Yuko nani anayetujua?

16Mmepotea kabisa!

Uko udongo unaowaziwa kuwa sawa na mfinyanzi?

Au kiko kiumbe kiwezacho kumwambia aliyekiumba:

Hukunifanya?

Au kiko chombo kiwezacho kumwambia aliyekifinyanga:

Hujui kitu?

Bwana atayageuza yote.

17Sicho kitambo kidogo bado,

Libanoni kugeuke kuwa shamba,

nayo mashamba yawaziwe kuwa mwitu?

18*Siku ile viziwi watayasikia maneno yaliyoandikwa,

nayo macho ya vipofu yaliyokuwa yenye giza jeusi yataona.

19Nao wanyonge wataendelea kumfurahia Bwana

nao walio wakiwa kuliko watu wengine

watamshangilia Mtakatifu wa Isiraeli.

20Kwani wakorofi watakuwa wamekwisha,

nao wafyozaji watakuwa wameangamia,

nao wote watakuwa wameng'olewa

waliokataa kulala usingizi, wapate kuwapotoa wenzao.

21Ndio wanaokosesha wengine shaurini,

ndio wanaowategea waamuliao penye malango ya mji,

kwani hivyo wanawapotoa waongofu, wasishinde shaurini.*

22Kwa sababu hii Bwana alimkomboa Aburahamu,

akauambia mlango wa Yakobo:

Sasa Yakobo hatapatwa tena na soni,

wala uso wake hautamvilia tena.

23Kwani watoto wake watakapoona,

mikono yangu itakayoyafanya kwao,

watalitakasa Jina langu,

ndiko kumtakasa Mtakatifu wa Yakobo

na kumcha Mungu wa Isiraeli.

24Ndipo, waliopotea rohoni watakapojua utambuzi

nao walionung'unika watajifundisha yafaayo.

Swahili Roehl Bible 1937 © Bible Society of Tanzania, 1937.
Published by: Bible Society of Tanzania