Ufunuo 6

Maana ya muhuri saba: 1. Mpanda farasi mweupe.

1Kisha nikamwona Mwana kondoo, akifungua moja ya zile muhuri saba. Nikasikia, mmoja wa wale nyama wanne akisema kama kwa sauti ya ngurumo: Njoo![#Ufu. 4:6-8; 5:1-2,6,8.]

2Nikatazama, nikaona farasi mweupe, naye aliyempanda alikuwa na uta, akapewa kilemba; kisha yeye aliyekuwa mshindaji akatoka, ashinde tena.[#Zak. 1:8; 6:1-5.]

2. Mpanda farasi mwekundu.

3Alipoifungua muhuri ya pili, nikasikia, nyama wa pili akisema: Njoo![#Ufu. 4:7.]

4Pakatokea farasi mwingine, ni mwekundu sana; aliyempanda akapewa kuuondoa utengemano katika nchi, wapate kuuana wao kwa wao. Naye akapewa upanga mkubwa.

3. Mpanda farasi mweusi.

5Alipoifungua muhuri ya tatu, nikasikia, nyama wa tatu akisema: Njoo! Nikatazama, nikaona farasi mweusi, naye aliyempanda alikuwa na kipimo mkononi mwake.[#Ufu. 4:7.]

6Nikasikia iliyokuwa kama sauti iliyokuwa katikati ya wale nyama wanne, ikisema: Kibaba cha mchele ni shilingi, vibaba vitatu vya mtama ni shilingi. Lakini mafuta usiyapotoe, wala mvinyo!

4. Mpanda farasi mwenye rangi ya kijivujivu.

7Alipoifungua muhuri ya nne, nikasikia, nyama wa nne akisema: Njoo![#Ufu. 4:7.]

8Nikatazama, nikaona farasi wa kijivujivu, naye aliyempanda jina lake Kifo, nao wazimu wakafuatana naye. Wakapewa nguvu ya fungu la nne la nchi, wawaue kwa panga na kwa njaa na kwa magonjwa yauayo na kwa nyama wakali waliopo nchini.[#Yer. 15:3; Ez. 14:21.]

5. Roho zao waliouawa kwa ajili ya Neno la Mungu.

9Alipoifungua muhuri ya tano, nikaona, mvunguni mwa meza ya Bwana zimo roho zao waliouawa kwa ajili ya Neno la Mungu na kwa ajili ya ushuhuda, walioushuhudia.[#Ufu. 8:5; 14:18; 16:7.]

10Nao wakalia kwa sauti kuu wakisema: Mpaka lini, wewe Bwana uliye mtakatifu na mkweli? Mbona huwahukumu wanaokaa nchini, uzilipize damu zetu?[#Ufu. 18:10; 1 Mose 4:10.]

11Ndipo, walipopewa kila mmoja kanzu nyeupe, wakaambiwa, wanyamaze siku chache tena, mpaka yatimilike mambo ya watumwa wenzao nayo ya ndugu zao watakaouawa vivyo hivyo kama wao wenyewe.[#Ufu. 3:4-5; 7:9,13-14.]

6. Siku kubwa ya makali.

12Nikamwona, alipoifungua muhuri ya sita. Pakawa tetemeko kubwa la nchi, hata jua likawa jeusi kama gunia la makonge, mwezi wote ukawa kama damu,[#Yes. 13:10; Yoe. 2:30-31; Mat. 24:29; Luk. 21:25.]

13nyota za mbinguni zikaanguka nchini, kama mkuyu unavyoyabwaga mapooza yake ukitikiswa na upepo mwingi.[#Yes. 34:4.]

14Kisha mbingu zikatengeka kama karatasi linalojizinga upesi, hata milima yote na visiwa vyote vikaondolewa mahali pao.

15Ndipo, wafalme wa nchini, nao walio wakubwa, nao wakuu wa vikosi, nao wenye mali, nao wenye nguvu, nao watumwa wote, nao waungwana wote walipojificha mapangoni na miambani penye milima[#Yes. 2:10,19.]

16wakiiambia milima na miamba: Tuangukieni, mtufiche machoni pake yeye anayekaa kitini mwa kifalme napo penye makali ya Mwana kondoo![#Luk. 23:30.]

17Kwani imekuja siku kubwa ya makali yao, yuko nani awezaye kusimama?[#Rom. 2:5.]

Swahili Roehl Bible 1937 © Bible Society of Tanzania, 1937.
Published by: Bible Society of Tanzania