Amosi 2

Amosi 2

Moabu

1Mwenyezi-Mungu asema hivi:

“Watu wa Moabu wametenda dhambi tena na tena,

kwa hiyo sitaacha kuwaadhibu.

Wamemkosea heshima marehemu mfalme wa Edomu

kwa kuichoma moto mifupa yake

ili kujitengenezea chokaa!

2Basi, nitaishushia moto nchi ya Moabu,

na kuziteketeza kabisa ngome za mji wa Keriothi.

Wanajeshi watakapopaza sauti zao na kupiga tarumbeta,

watu wa Moabu watakufa katika makelele hayo ya vita.

3Isitoshe, nitamuua mtawala wa Moabu,

pamoja na viongozi wote wa nchi hiyo.

Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”

Yuda

4Mwenyezi-Mungu asema hivi:

“Watu wa Yuda wametenda dhambi tena na tena,

kwa hiyo sitaacha kuwaadhibu.

Wamepuuza sheria zangu,

wala hawakufuata amri zangu.

Wamepotoshwa na miungu ileile waliyoihudumia wazee wao.

5Basi, nitaishushia moto nchi ya Yuda,

na kuziteketeza kabisa ngome za Yerusalemu.”

Hukumu ya Mungu juu ya Israeli

6Mwenyezi-Mungu asema hivi:

“Waisraeli wametenda dhambi tena na tena,

kwa hiyo sitaacha kuwaadhibu.

Wamewauza watu waaminifu

kwa kuwa hawakuweza kulipa madeni yao;

na kuwauza watu fukara

wasioweza kulipa deni la kandambili.

7Huwanyanyasa na kuwakandamiza wanyonge,

na maskini huwabagua wasipate haki zao.

Mtu na baba yake hulala na mjakazi yuleyule,

hivyo hulitia unajisi jina langu takatifu.

8Popote penye madhabahu,

watu hulalia nguo walizotwaa kwa maskini

kama dhamana ya madeni yao;

na katika nyumba ya Mungu wao

hunywa divai waliyotwaa kwa wadeni wao.

9“Hata hivyo, enyi watu wangu,

kwa ajili yenu, niliwaangamiza kabisa Waamori

ambao walikuwa wakubwa kama mierezi,

wenye nguvu kama miti ya mialoni.

Naam, niliwaangamiza, matawi na mizizi.

10Niliwatoeni kutoka nchi ya Misri,

nikawaongoza kupitia jangwani miaka arubaini,

mpaka mkaichukua nchi ya Waamori kuwa yenu.

11Niliwateua baadhi ya wana wenu wawe manabii,

na baadhi ya vijana wenu wawe wanadhiri.

Je, enyi Waisraeli,

haya nisemayo si ya kweli?

Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.

12Lakini nyinyi mliwafanya wanadhiri wanywe divai,

na kuwaamuru manabii wasitoe unabii.

13“Sasa basi, nitawagandamiza mpaka chini,

kama gari lililojaa nafaka.

14Hata wapiga mbio hodari hawataweza kutoroka;

wenye nguvu wataishiwa nguvu zao,

na askari watashindwa kuyaokoa maisha yao.

15Wapiga upinde vitani hawatastahimili;

wapiga mbio hodari hawataweza kujiokoa,

wala wapandafarasi hawatayanusurisha maisha yao.

16Siku hiyo, hata askari hodari

watatimua mbio bila chochote.

Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote (Yenye Vitabu vya Deuterokanoni): Tafsiri ya Ushirikiano wa Makanisa (BHN): Hakimiliki -1995, 2001: kwa Chama cha Biblia cha Tanzania na Chama cha Biblia cha Kenya. Haki zote zimehifadhiwa.
Published by: Bible Society of Tanzania