The chat will start when you send the first message.
1Kumbuka kwamba, katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za taabu.[#3:1 Yaani nyakati au siku zitakazotangulia kurudi kwake Yesu Kristo. Kwamba siku hizo za mwisho zitakuwa za taabu taz Mat 24; Marko 13; 2Thes 2:3-12.]
2Watu watakuwa na ubinafsi, wenye tamaa ya fedha, wenye majivuno, wenye kujiona, wenye kumtukana Mungu, wasiowatii wazazi wao, wasio na shukrani na waovu;
3watatokea watu wasio na upendo moyoni, wasio na huruma, wachongezi, walafi na wakali; watachukia chochote kilicho chema;
4watakuwa wahaini, wakaidi na waliojaa kiburi; watapenda anasa kuliko kumpenda Mungu.
5Kwa nje wataonekana kama watu wenye kumcha Mungu, lakini wataikana nguvu yake. Jiepushe kabisa na watu wa namna hiyo.
6Baadhi yao huenda katika nyumba za watu na huwateka wanawake dhaifu waliolemewa mizigo ya dhambi na ambao wanaongozwa na tamaa za kila aina;
7wanawake ambao wanajaribu daima kujifunza lakini hawawezi kuufikia ujuzi wa huo ukweli.
8Watu hao huupinga ukweli kama vile Yane na Yambre walivyompinga Mose. Hao ni watu wa akili potovu na imani ya uongo.[#3:8 Majina haya yametajwa katika mapokeo ya Kiyahudi ambayo yamewapa majina hayo wale wachawi wanaotajwa katika Kut 7:11-12,22; 9:11.]
9Lakini hawataweza kuendelea zaidi kwa maana upumbavu wao utaonekana wazi kwa wote. Ndivyo ilivyokuwa kwa akina Yane na Yambre.
10Wewe, lakini, umeyafuata mafundisho yangu, mwenendo wangu, makusudi yangu katika maisha, imani yangu, uvumilivu wangu, upendo wangu, subira yangu,
11udhalimu na mateso. Unayajua mambo yaliyonipata huko Antiokia, Ikonio na Lustra. Nilivumilia udhalimu mkubwa mno! Lakini Bwana aliniokoa katika mambo hayo yote.[#3:11 Rejea Zab 34:19.]
12Kila mtu anayetaka kuishi maisha ya kumcha Mungu katika kuungana na Kristo Yesu lazima adhulumiwe.[#3:12 Rejea Mat 5:10-11; Yoh 15:20; Mate 14:22.]
13Watu waovu na wadanganyifu wataendelea kuwa wabaya, wakidanganya wengine, na wao wenyewe wakidanganywa.
14Lakini wewe dumu katika ukweli ule uliofundishwa ukaukubali kabisa. Wawajua wale waliokuwa waalimu wako,[#3:14 Au: “wewe wajua ulijifunza kutoka kwa akina nani”. Maneno ambayo labda yanamhusu Paulo mwenyewe (2Tim 2:2) au hata wengine kama akina mama Loisi na Eunike (2Tim 1:5).]
15wakumbuka kwamba tangu utoto wako umejua Maandiko Matakatifu ambayo yaweza kukupatia hekima iletayo wokovu kwa njia ya imani kwa Kristo Yesu.
16Maandiko yote Matakatifu yameandikwa kwa uongozi wa Mungu, na yanafaa katika kufundishia ukweli, kuonya, kusahihisha makosa, na kuwaongoza watu waishi maisha adili,[#3:16 Kuhusu maneno “kwa uongozi wa Mungu” rejea Ebr 4:12; 2Pet 1:21. Neno linalotafsiriwa “kwa uongozi” katika Kigiriki ni neno linaloashiria kitendo cha “kupuliza”, nalo latumika kutilia mkazo chanzo cha hayo Maandiko Matakatifu, kwa hiyo yameongozwa na Mungu.]
17ili mtu wa Mungu awe mkamilifu, na tayari kabisa kufanya kila kazi njema.[#3:17 Taz 1Tim 6:11.]