Zaburi 146

Zaburi 146

Sifa kwa Mungu Mwokozi

1Msifuni Mwenyezi-Mungu![#146:1 Zaburi zote 146-150 huanza na kumalizia kwa mwito huo.]

Umsifu Mwenyezi-Mungu, ee nafsi yangu!

2Nitamsifu Mwenyezi-Mungu maisha yangu yote;

nitamwimbia Mungu wangu muda wote niishipo.

3Msiwategemee wakuu wa dunia;[#146:3 Tamko hili ni ujumbe mahsusi kabisa ambao ulitiliwa maanani na Wanazaburi (Zab 118:8-9) na manabii (Isa 2:22; 31:3; Yer 17:5). Lengo lake ni kwamba binadamu lazima aweke tegemeo lake kwa Mungu na sio kwa binadamu, mali, miungu n.k.]

hao ni binadamu tu, hawawezi kuokoa.

4Binadamu akitoa pumzi yake ya mwisho,

anarudi mavumbini alimotoka;

na hapo mipango yake yote hutoweka.

5Heri mtu anayesaidiwa na Mungu wa Yakobo,

mtu aliyeweka tumaini lake kwa Mwenyezi-Mungu, Mungu wake,

6aliyeumba mbingu na dunia,

bahari na vyote vilivyomo.

Yeye hushika ahadi yake milele.

7Yeye huwapatia wanaoonewa haki zao,

huwapa wenye njaa chakula.

Mwenyezi-Mungu huwapa wafungwa uhuru,

8huwafungua macho vipofu.

Mwenyezi-Mungu huwainua waliokandamizwa;

huwapenda watu walio waadilifu.

9Mwenyezi-Mungu huwalinda wageni,

huwategemeza wajane na yatima;

lakini huipotosha njia ya waovu.

10Mwenyezi-Mungu atawala milele,

Mungu wako, ee Siyoni, ni mfalme vizazi vyote!

Msifuni Mwenyezi-Mungu!

Copyright The Bible Society of Tanzania, 1993 The Bible Society of Kenya 1993
Published by: Bible Society of Tanzania