Zaburi 22

Zaburi 22

Kilio

1Mungu wangu, Mungu wangu, mbona umeniacha?[#22:1 Swali la namna hii hutokea mara nyingi katika sala za kumwomba Mungu msaada katika hali ngumu. Mtunzi wa Zaburi hii anajikuta katika upeo wa mateso kiasi cha kuona kwamba ahadi ya Mungu (kwa mfano Yos 1:7 ambapo Mungu anaahidi kwamba hatamwacha mtumishi wake) imetoweka na hana la kufanya ila kilio kwa Mungu wake. Wakati maalumu ulipofika, Yesu alitumia kilio hicho (Mat 27:46; Marko 15:34) alipofikia upeo wa mateso aliyoyakubali ili awaokoe watu wa Mungu.]

Mbona uko mbali sana kunisaidia,

mbali na maneno ya kilio changu?

2Ee Mungu wangu, nalia mchana lakini hujibu;

napiga yowe usiku, lakini nafuu sipati.

3Hata hivyo, wewe ni mtakatifu;

wewe watawala na kusifiwa na Waisraeli.

4Wazee wetu walikutegemea;

walikutegemea, nawe ukawaokoa.

5Walikulilia wewe, wakaokolewa;

walikutegemea, nao hawakuaibika.

6Lakini mimi ni mdudu tu, wala si mtu;

nimepuuzwa na kudharauliwa na watu.

7Wote wanionao hunidhihaki;

hunifyonya na kutikisa vichwa vyao.

8Husema: “Alimtegemea Mwenyezi-Mungu,

basi, Mungu na amkomboe!

Kama Mungu anapendezwa naye,

basi, na amwokoe!”

9Lakini ndiwe uliyenitoa tumboni mwa mama yangu,

uliniweka salama kifuani pa mama yangu.

10Nimekutegemea tangu kuzaliwa kwangu.

Tangu nilipozaliwa wewe umekuwa Mungu wangu.

11Usikae mbali nami, kwani taabu imekaribia;

wala hakuna wa kunisaidia.

12Maadui wengi wanizunguka kama fahali;[#22:12-13 Mtunzi wa Zaburi anaeleza kuhusu maadui zake walio kama wanyama wakali (taz pia 22:16,20-21). Hao wanyama wanaotajwa wana nguvu kuliko binadamu.]

wamenisonga kama fahali wakali wa Bashani!

13Wanafunua vinywa vyao kama simba,

tayari kushambulia na kurarua.

14Nimekwisha kama maji yaliyomwagika;

mifupa yangu yote imeteguka;

moyo wangu ni kama nta,

unayeyuka ndani mwangu.

15Koo langu limekauka kama kigae;

ulimi wangu wanata kinywani mwangu.

Umeniacha kwenye mavumbi ya kifo.

16Genge la waovu limenizunguka;

wananizingira kama kundi la mbwa;

wamenitoboa mikono na miguu.

17Nimebaki mifupa mitupu;

maadui zangu waniangalia na kunisimanga.

18Wanagawana nguo zangu,

na kulipigia kura vazi langu.

19Lakini wewe ee Mwenyezi-Mungu, usikae mbali nami;

ewe msaada wangu, uje haraka kunisaidia.

20Iokoe nafsi yangu mbali na upanga,

yaokoe maisha yangu makuchani mwa mbwa hao!

21Uniokoe kinywani mwa simba;

iokoe nafsi yangu dhaifu toka pembe za nyati hao.

Wimbo wa shukrani

22Nitawasimulia ndugu zangu matendo yako;

nitakusifu kati ya kusanyiko lao:

23Enyi mnaomcha Mwenyezi-Mungu, msifuni!

Mtukuzeni enyi wazawa wote wa Yakobo!

Mcheni Mungu enyi wazawa wote wa Israeli!

24Maana yeye hapuuzi au kudharau unyonge wa mnyonge;

wala hajifichi mbali naye,

ila humsikia anapomwomba msaada.

25Kwa sababu yako ninakusifu

katika kusanyiko kubwa la watu;

nitatimiza ahadi zangu mbele yao wakuchao.

26Maskini watakula na kushiba;

wanaomtafuta Mwenyezi-Mungu watamsifu.

Mungu awajalie kuishi milele!

27Ulimwengu wote utakumbuka na kumrudia Mwenyezi-Mungu;

jamaa zote za mataifa zitamwabudu.

28Maana Mwenyezi-Mungu ni mfalme;

yeye anayatawala mataifa.

29Wenye kiburi wote duniani watasujudu mbele yake;

wote ambao hufa watainama mbele yake,

wote ambao hawawezi kudumisha uhai wao.

30Vizazi vijavyo vitamtumikia;

watu watavisimulia habari za Mwenyezi-Mungu,

31watatangaza matendo yake ya wokovu.

Watu wasiozaliwa bado wataambiwa:

“Mwenyezi-Mungu ndiye aliyefanya hayo!”

Copyright The Bible Society of Tanzania, 1993 The Bible Society of Kenya 1993
Published by: Bible Society of Tanzania