Waroma 11

Waroma 11

Huruma ya Mungu kwa Israeli

1Basi, nauliza: je, Mungu amewakataa watu wake? Hata kidogo! Mimi binafsi ni Mwisraeli, mzawa wa Abrahamu, wa kabila la Benyamini.[#11:1 Mfalme wa kwanza wa Waisraeli alikuwa pia wa kabila la Benyamini. Benyamini ambaye kabila hilo lilijulikana kwa jina lake, alikuwa mtoto wa mwisho wa Yakobo (Israeli).]

2Mungu hakuwakataa watu wake aliowateua tangu mwanzo. Mnakumbuka yasemavyo Maandiko Matakatifu juu ya Elia wakati alipomnung'unikia Mungu kuhusu Israeli:[#11:2-3 Huyu aliishi karibu miaka 800 K.K. Alikuwa nabii wakati wa mfalme Ahabu, wakati ambapo Waisraeli, kwa wingi, walimwacha Mungu na kuifuata miungu ya watu wa Kanaani (1Fal 16:29—19:18).]

3“Bwana, wamewaua manabii wako na kubomoa madhabahu yako. Ni mimi tu peke yangu niliyebaki, nao wanataka kuniua!”

4Je, Mungu alimjibu nini? Alimwambia: “Nimejiwekea watu 7,000 ambao hawakumwabudu Baali.”[#11:4 Huyu alikuwa mmojawapo wa miungu ya watu wa Kanaani. Jina lake lina maana ya “Bwana”.]

5Basi, ndivyo ilivyo pia wakati huu wa sasa: ipo idadi ya waliobaki ambao Mungu aliwateua kwa sababu ya neema yake.[#11:5-7 Maelezo juu ya neema na wateule wanaobaki bila kuangamizwa yanasisitiza mkazo wa Paulo kuhusu mtu kuhesabiwa mwadilifu kwa imani ambao umo katika barua nzima (taz pia 9:29).]

6Uteuzi wake unatokana na neema yake, na si kwa sababu ya matendo yao. Maana, kama uteuzi wake ungetegemea matendo ya watu, neema yake haingekuwa neema tena.

7Sasa, je? Watu wa Israeli hawakukipata kile walichokuwa wanakitafuta; lakini wote walioteuliwa walikipata. Wengine walipumbazwa,[#11:7-10 Maelezo juu ya Waisraeli wa aina mbili: wateule waadilifu na wale wasio waadilifu.; #11:7 Njia yake Paulo ya kuamsha nia ya wasomaji wa barua yake.; #11:7 Yaani wokovu unaotolewa kwa neema kwa kumwamini Mwana wa Mungu jambo ambalo ni chukizo kwa wale wasiomwamini (taz pia 8:29-30).; #11:7-8 Ni kama vile inavyoelezwa katika aya 8 maneno ambayo ni nukuu kutoka Isa 6:9-10; 29:10; Kumb 29:4.]

8kama yasemavyo Maandiko Matakatifu:

“Mungu ameifanya mioyo yao kuwa mizito,

na mpaka leo hii hawawezi kuona kwa macho yao

wala kusikia kwa masikio yao.”

9Naye Daudi anasema:

“Karamu zao na ziwe mtego wa kuwanasa,

waanguke na kuadhibiwa.

10Macho yao yatiwe giza

wasiweze kuona.

Migongo yao ipindike kwa taabu daima!”

11Basi, nauliza: je, Wayahudi wamejikwaa hata wakaangamia kabisa? Hata kidogo! Kutokana na kosa lao ukombozi umewajia watu wa mataifa mengine, ili Wayahudi wapate kuwaonea wivu.[#11:11 Paulo anataka kuonesha kuwa tendo la Wayahudi kuwaonea wivu wale wasio Wayahudi kwa kupata wokovu ni utimilifu wa maneno ya unabii ya Mose (Kumb 32:21; taz pia Rom 10:19). na wa kiroho ni kule kutomwamini Yesu Kristo (taz 10:17).]

12Kosa la Wayahudi limesababisha baraka nyingi kwa ulimwengu, na utovu wao wa kiroho umeleta baraka nyingi kwa watu wa mataifa mengine. Basi, ni dhahiri kwamba kuingizwa kwa idadi yao kamili kutakuwa ni baraka zaidi.[#11:12 Au “Baraka nyingi kwa watu wote.” Wale wasio Wayahudi wanapata wokovu ambao wao Wayahudi wameupuuza kwa kutokuamini “Habari Njema” kuwa Kristo ni Mwana wa Mungu na Mwokozi na kila aaminiye awe Myahudi au asiwe Myahudi (taz 10:5-13,16).; #11:11-12 Paulo anakaza hasara kwa Wayahudi wasioamini na faida kwa wale wasio Wayahudi. Mkazo wake wa kuonesha kuwa Mungu hana ubaguzi (taz pia 9:2,30,32; 10:11-13). Hata wale ambao hapo awali hawakuwa na uhusiano naye kwa njia ya agano, sasa kwa kumwamini Yesu Kristo wamehesabika kati ya watoto wake (taz tena 9:8,30-32).]

Ukombozi wa watu wa mataifa mengine

13Basi, sasa nawaambieni nyinyi watu wa mataifa mengine: Maadamu mimi nimekuwa mtume kwa watu wa mataifa mengine, ninajivunia huduma yangu,[#11:13 Ni msemo unaorudiwa mara nyingi katika barua hii akiwataja hao wasio Wayahudi.; #11:13 Paulo mara kwa mara anajitaja kwa cheo hicho katika barua zake ili kukaza kuwa yeye kazi yake ilikuwa kuwaendea wasio Wayahudi, kazi ambayo aliiendeleza; kwani hakuwa wa kwanza kufanya hivyo (taz Mate 9:15,17-22; 11:1; Kumb 1:5; Gal 1:16; 2:7,9).]

14nipate kuwafanya wananchi wenzangu wawaonee nyinyi wivu, na hivyo nipate kuwaokoa baadhi yao.[#11:14 Taz Kumb 32:21; Rom 10:19; 11:11.; #11:14 Yaani awahubiri Injili wapate kuamini. Hapa anaeleza shabaha ya wito alioitiwa (taz Mate 9:5-6,15-16).]

15Maana ikiwa kukataliwa kwao kulisababisha ulimwengu upatanishwe na Mungu, itakuwaje wakati watakapokubaliwa na Mungu? Wafu watafufuka![#11:15 Mungu hakuwakataa kabisa bali walipotenda dhambi aliwaacha akiwapa muda watubu wamrudie. Kwa ajili ya uasi wao na kutotii kwao alimtuma Mwokozi ili wao hata na watu wengine ulimwenguni wapatanishwe naye, yaani waumini, wawe watoto wake, mkazo wa Paulo katika barua nzima (taz pia 8:14-17).; #11:15 Msemo ambao unaweza ukawa na maana mbalimbali, k.m. kufufuka kiroho (taz Zab 51:10; Eze 36:26; 37:7-14; 1 Kor 3:18). Kufufuka kimwili; hii ni kufuatana na jinsi Yesu Kristo alivyotabiri (taz Yoh 11:21-26a; 5:29; 6:40; Luka 14:14; ling Yoh 3:16; Yobu 19:25; 1 Kor 15:13,21,42; Dan 12:2). Kufufuka kunakotajwa kuna lugha ya kimfano, Paulo akiwaelezea Warumi kuwa Wayahudi wakitubu na kuamini watapata maisha mapya na kwa njia hiyo watatambua umuhimu wa kutoka kuvuka mipaka yao watangaze “Habari Njema” kama mitume walivyofanya.]

16Ikiwa kipande cha kwanza cha mkate kimewekwa wakfu, mkate wote umewekwa wakfu; mizizi ya mti ikiwa mizuri, na matawi yake huwa mazuri pia.[#11:16 Lugha ya kimfano. Paulo anaonesha ujumla wa vitu. Kwa mifano hiyo anawafananisha Waisraeli na wakati walipokuwa wakitii.]

17Naam, baadhi ya matawi ya mzeituni bustanini yalikatwa, na mahali pake tawi la mzeituni mwitu likapandikizwa. Nyinyi watu wa mataifa mengine ndio hilo tawi la mzeituni mwitu; na sasa mnashiriki nguvu na utomvu wa mzeituni bustanini.[#11:17-24 Lugha ya kimfano inatumika hapa kuwafundisha na kuwaonya ambao si watu wa agano - yaani si Wayahudi au si wazawa wa Abrahamu kimwili; ili wakae kwa amani na Wayahudi, na wajione kuwa wako bora kuliko hao wazawa wa Abrahamu kimwili lakini bila imani.]

18Basi, msiwadharau wale waliokatwa kama matawi! Na, hata kama kuna la kujivunia, kumbukeni kwamba si nyinyi mnaoitegemeza mizizi, bali mizizi ndiyo inayowategemeza nyinyi.

19Lakini utasema: “Matawi yalikatwa kusudi mimi nipandikizwe mahali pake.”

20Sawa! Yalikatwa kwa sababu ya kukosa imani, bali wewe unasimama kwa imani yako. Lakini usijivune; ila uwe na tahadhari.[#11:20 Tafsiri nyingine Kuwa na tahadhari kulisisitizwa katika Agano la Kale na kulikuwa fundisho la hekima (taz k.m. Mwa 20:11; Yobu 28:28; Zab 111:10; 112:1; Meth 1:7; 3:7; Mhub 12:13; Fil 2:12-13; Ebr 4:1; 1Pet 1:17).]

21Kwa maana, ikiwa Mungu hakuwahurumia Wayahudi ambao ni kama matawi ya asili, je, unadhani atakuhurumia wewe?[#11:21 Paulo anakumbusha wasomaji wa barua yale yaliyotendeka katika historia nzima ya wokovu. Walipomkosea Mungu naye aliharibu nchi yao au aliwapeleka utumwani, n.k., mfano ni walipotoka Misri; walimkosea Bwana njiani, wakapaswa kusafiri kwa miaka arubaini ambapo wangefika kwa siku chache.; #11:21 Namna nyingine ya kuita taifa la Israeli lililochaguliwa na Mungu.]

22Ona, basi, jinsi Mungu alivyo mwema na mkali. Yeye ni mkali kwa wale walioanguka, na ni mwema kwako wewe ikiwa utaendelea katika wema wake; la sivyo, nawe pia utakatwa.[#11:22 taz maelezo ya 2:4. Mkali yaani hapendi ubaya. Hii ni tangu mwanzo Adamu na Hawa walipoanguka dhambini, Mungu aliwatangazia laana na kuwafukuza toka bustani ya Edeni (taz Mwa 3:1-24; 5; 9; 11:1-9).]

23Nao Wayahudi, hali kadhalika; wakiacha utovu wao wa imani, watapandikizwa tena. Maana Mungu anao uwezo wa kuwapandikiza tena.[#11:23 Ling aya ya 15.]

24Nyinyi watu wa mataifa mengine, kwa asili ni kama tawi la mzeituni mwitu, lakini mmeondolewa huko, mkapandikizwa katika mzeituni bustanini mahali ambapo kwa asili si penu. Lakini, Wayahudi kwa asili ni kama mzeituni bustanini, na itakuwa jambo rahisi zaidi kwao kupandikizwa tena katika mti huohuo wao.[#11:24 Wayahudi ndio waliochaguliwa wakatumainishiwa Masiha - Mkombozi; shabaha ni ili mataifa mengine yaokolewe kwa njia ya hao wazawa wa Abrahamu. Kwa hiyo huko kupandikizwa ni mtu kufanywa mwadilifu kwa imani yake, na kuitwa mtoto wa Mungu.; #11:24 Taz aya 15,23. Paulo ingawa anatumia lugha kali kwa Wayahudi, lakini bado anatoa mkazo wa matumaini ya kuhurumiwa na kusamehewa na kuwaita watoto wake tena; ndiyo sababu anasisitiza huruma ya Mungu akimwita (taz tena aya 22; Kut 34:6-7; 2Nya 30:9; Zab 103:8; 117:2; Yoe 2:15; Yona 4:2; Yer 3:12; ling Mat 19:26; Marko 10:27; 18:27).; #11:24 Onyo kwa wasio wazawa wa Abrahamu ndio hao]

Kuongoka kwa Israeli

25Ndugu zangu, napenda mjue ukweli huu uliofichika msije mkajiona wenye akili sana. Ukaidi wa Wayahudi ulikuwa ni wa muda tu, mpaka watu wa mataifa mengine watakapokuwa wamemfikia Mungu.[#11:25 Taz maelezo ya 10:1; #11:25 Amekwisha waonya waepukane na majivuno (taz aya ya 18).; #11:25 Ni kama mkazo huohuo uliomo katika aya ya 15,24.; #11:25 Muda kimiaka hautajwi bali wa kimatukio.]

26Hapo ndipo taifa lote la Israeli litakapookolewa, kama yasemavyo Maandiko Matakatifu:

“Mkombozi atakuja kutoka Siyoni,

atauondoa uovu wa wazawa wa Yakobo.

27Hili ndilo agano nitakalofanya nao

wakati nitakapoziondoa dhambi zao.”

28Kwa sababu wanaikataa Habari Njema, Wayahudi wamekuwa maadui wa Mungu, lakini kwa faida yenu nyinyi watu wa mataifa. Lakini, kwa kuwa waliteuliwa, bado ni marafiki wa Mungu kwa sababu ya babu zao.[#11:28 Yaani wakosapo Mungu hawatupi kabisa bado kuna matumaini kuwa watamrudia.; #11:28 Hao wakina Abrahamu, Isaka na Yakobo.]

29Maana Mungu akisha wapa watu zawadi zake na kuwateua, hajuti kwamba amefanya hivyo.

30Hapo awali nyinyi mlikuwa mmemwasi Mungu, lakini sasa mmepata huruma yake kutokana na kuasi kwao.[#11:30-32 Marudio ya yale ambayo amekwisha sema taz aya 12,15,17. Jambo la Wayahudi kupata huruma yake Mungu ni kufuatana na mpango ya kwamba taifa lote halikutupwa kabisa, bali Mungu yu tayari kuwapokea ikiwa watamrudia; kutii na kutenda kufuatana na matakwa yake. Mkazo uliomo katika mistari hii unapatana na ule uliomo katika 9:25-26,29 na pia 11:12b; unaosisitiza kuwa Mungu mara kwa mara ameacha baadhi ya Waisraeli wasiangamie.]

31Hali kadhalika, kutokana na huruma mliyojaliwa nyinyi, Wayahudi wanamwasi Mungu sasa ili nao pia wapokee sasa huruma ya Mungu.

32Maana Mungu amewafunga watu wote katika uasi wao ili apate kuwahurumia wote.[#11:32 Ni mkazo wa Paulo kuwa Wayahudi na wasio Wayahudi. Mungu anaona uasi wao na yu tayari kuwapa adhabu bila ubaguzi. Hivyo Wayahudi wasijione kuwa bora kwa kuwa ni wa uzao wa Abrahamu kimwili (ling 9:15-18; 11:8-10; taz Isa 6). Lengo la Paulo ni kuonesha kuwa watu wote ni wenye dhambi — mkazo ambao amekwisha utoa katika 3:9-20,23,25; 5:8,12; 6:20-21; 8:10.]

Mungu asifiwe

33Utajiri, hekima na elimu ya Mungu ni kuu mno! Huruma zake hazichunguziki, na njia zake hazieleweki! Kama yasemavyo Maandiko Matakatifu:[#11:33 Taz 10:12.; #11:33 Katika mafundisho ya Wayahudi ilisisitizwa kuwa Mungu ndiye mwenye ya kweli, ndiye anayefahamu ilipo, na ndiye mwenye kuwatia watu ifaayo. Katika kazi zake zote hutumia hata tangu wakati wa kuumba (taz pia Yobu 28:20-27; Zab 37:30; 51:6; 111:10; 119:98; Meth 2:6; 3:19; ling 1Fal 4:29).; #11:33 Au Mafundisho ya Mungu au sheria za Mungu au kazi nzima yake Mungu. Hii ni jinsi zilivyoelezwa katika vitabu vitano vya mwanzoni yaani; #11:33 Ni kama anasisitiza kuwa hali ya Mungu ni kuwa na anasema hivyo mara nyingi katika barua yote - taz pia 9:15,23. Yu tayari kuhurumia Wayahudi na wasio Wayahudi. Yaani zake hazina mipaka. Ili kukaza zake Mungu zisivyo za kawaida ndiyo sababu anazieleza kuwa halafu anaongeza maneno na Huo ni kama mkazo mpya usiopatana na mawazo ya Wayahudi wengi ambao walipingana naye Paulo.]

34“Nani aliyepata kuyajua mawazo ya Bwana?

Nani awezaye kuwa mshauri wake?

35Au, nani aliyempa yeye kitu kwanza

hata aweze kulipwa tena kitu hicho?”

36Kwa maana vitu vyote vyatoka kwake, vyote vipo kwa uwezo wake na kwa ajili yake. Utukufu na uwe kwake hata milele! Amina.[#11:36 Mkazo kuwa yeye ni Mungu wa maumbile, kwa hiyo yu huru kuvitumia apendavyo (taz aya ya 33).; #11:36 Marudio aliyokwisha sema katika aya zilizotangulia yaani 33-35, hapa akikazia uhusiano wake na vitu vyenyewe. Kwa jumla ni kwamba hivyo alivyoumba au hivyo alivyo navyo huvitumia kwa mapenzi yake mwenyewe.; #11:36 Namna yake Paulo ya kumalizia sehemu kuu katika barua zake (taz pia Gal 1:5; Efe 3:20-21; 4:20; 1Tim 1:17; 6:16; 2Tim 4:18).]

Copyright The Bible Society of Tanzania, 1993 The Bible Society of Kenya 1993
Published by: Bible Society of Tanzania