Zekaria 5

Zekaria 5

Maono ya sita: Kitabu kinachoruka

1Nilipotazama tena niliona kitabu kinaruka angani.[#5:1 Kitabu hicho cha namna ya msokoto (au gombo) cha ngozi au papiri kilikuwa ni mfano wa neno la Mungu (rejea Eze 2:9-10; Ufu 5:1; 10:9-11). Yamkini vipimo vyake vikubwa sana (aya 2) ni sawa na vile vya ukumbi wa hekalu la Solomoni (1Fal 6:3).]

2Yule malaika akaniuliza, “Unaona nini?” Nami nikamjibu, “Ninaona kitabu kinaruka angani; urefu wake ni mita tisa na upana wake ni mita nne na nusu.”

3Basi, yeye akaniambia, “Ndani ya kitabu hicho kumeandikwa laana ambayo itaikumba nchi nzima. Upande mmoja imeandikwa kwamba wezi wote watafukuzwa nchini, na upande mwingine imeandikwa kwamba wote wenye kuapa uongo kadhalika watafanyiwa vivyo hivyo.[#5:3 Laana zinazosemwa zimo katika kitabu hicho zaweza kuhusu zile zinazotajwa katika Kumb 27:14-26; 28:15-19. Taz pia Kut 20:7,15.]

4Mwenyezi-Mungu wa majeshi asema kuwa yeye mwenyewe ataipeleka laana hiyo. Itapenya kila nyumba ya mwizi na kila nyumba ya mwenye kuapa uongo kwa kutumia jina lake; itakaa humo na kuteketeza nyumba hiyo yote, mbao na mawe.”

Maono ya saba: Mwanamke kapuni

5Yule malaika aliyeongea nami alinikaribia, akaniambia, “Hebu tazama uone kile kinachokuja.”

6Nami nikamwuliza, “Ni kitu gani hicho?” Naye akanijibu, “Hicho ni kikapu chenye makosa ya nchi nzima.”[#5:6 Kiebrania ni “efa” yaani kipimo ambacho kiliweza kuwa na lita 22. Lakini katika maono haya, kikapu hicho au “efa” hakina kipimo cha kawaida kama inavyodhihirika katika aya ya 7.; #5:6 Makala ya Kiebrania: “jicho”.]

7Kikapu chenyewe kilikuwa na mfuniko uliotengenezwa kwa risasi; kilifunuliwa, nami nikaona mwanamke ameketi humo ndani.

8Yule malaika akaniambia, “Mwanamke huyo anawakilisha uovu!” Kisha huyo malaika akamsukumia ndani ya kikapu mwanamke huyo na kukifunika.

9Nilipotazama juu, niliona wanawake wawili wanatokea kunijia; walikuwa wakirushwa na upepo, nao walikuwa na mabawa yenye nguvu kama ya korongo. Wanawake hao wakakiinua kile kikapu angani.

10Basi, nikamwuliza yule malaika aliyezungumza nami, “Wanakipeleka wapi kile kikapu?”

11Naye akaniambia “Wanakipeleka katika nchi ya Shinari. Huko watakijengea hekalu na litakapokuwa tayari, watakiweka kikapu hicho ndani.”[#5:11 Hili ni jina lingine la kale la Babuloni (rejea Mwa 11:2; taz pia Dan 1:2).]

Copyright The Bible Society of Tanzania, 1993 The Bible Society of Kenya 1993
Published by: Bible Society of Tanzania