The chat will start when you send the first message.
1Usifurahie, ee Israeli;
usishangilie kama mataifa mengine.
Kwa kuwa hukuwa
mwaminifu kwa Mungu wako;
umependa ujira wa kahaba kwenye kila sakafu
ya kupuria nafaka.
2Sakafu za kupuria nafaka na mashinikizo ya kukamulia divai
havitalisha watu,
divai mpya itawapungukia.
3Hawataishi katika nchi ya Bwana ,
Efraimu atarudi Misri
na atakula chakula
kilicho najisi huko Ashuru.
4Hawatammiminia Bwana sadaka ya divai
wala dhabihu zao hazitampendeza.
Dhabihu kama hizo zitakuwa kwao
kama mkate wa waombolezaji;
nao wote wazilao watakuwa najisi.
Chakula hiki kitakuwa kwa ajili yao wenyewe;
kisije katika Hekalu la Bwana .
5Mtafanya nini katika siku ya sikukuu zenu zilizoamriwa,
katika siku za sikukuu za Bwana ?
6Hata ikiwa wataokoka maangamizi,
Misri atawakusanya,
nayo Memfisi itawazika.
Hazina zao za fedha zitasongwa na michongoma,
nayo miiba itafunika mahema yao.
7Siku za adhabu zinakuja,
siku za malipo zimewadia.
Israeli na afahamu hili.
Kwa sababu dhambi zenu ni nyingi sana
na uadui wenu ni mkubwa sana,
nabii anadhaniwa ni mpumbavu,
mtu aliyeongozwa na Mungu
anaonekana mwendawazimu.
8Nabii, pamoja na Mungu wangu,
ndiye mlinzi juu ya Efraimu,
hata hivyo mitego inamngojea
katika mapito yake yote,
na uadui katika nyumba ya Mungu wake.
9Wamezama sana katika rushwa,
kama katika siku za Gibea.
Mungu atakumbuka uovu wao
na kuwaadhibu kwa ajili ya dhambi zao.
10“Nilipompata Israeli, ilikuwa kama
kupata zabibu jangwani;
nilipowaona baba zenu, ilikuwa kama kuona
matunda ya kwanza katika mtini.
Lakini walipofika Baal-Peori, walijiweka wakfu
kwa ile sanamu ya aibu,
nao wakawa najisi
kama kitu kile walichokipenda.
11Utukufu wa Efraimu utaruka kama ndege:
hakuna kuzaa, hakuna kubeba mimba,
hakuna kuchukua mimba.
12Hata wakilea watoto,
nitamuua kila mmoja.
Ole wao
nitakapowapiga kisogo!
13Nimemwona Efraimu, kama Tiro,
aliyeoteshwa mahali pazuri.
Lakini Efraimu wataleta
watoto wao kwa mchinjaji.”
14Wape, Ee Bwana ,
je, utawapa nini?
Wape tumbo zinazoharibu mimba
na matiti yaliyokauka.
15“Kwa sababu ya uovu wao wote huko Gilgali,
niliwachukia huko.
Kwa sababu ya matendo yao ya dhambi,
nitawafukuza katika nyumba yangu.
Sitawapenda tena,
viongozi wao wote ni waasi.
16Efraimu ameharibiwa,
mzizi wao umenyauka,
hawazai tunda.
Hata kama watazaa watoto,
nitawachinja wazao wao
waliotunzwa vizuri.”
17Mungu wangu atawakataa
kwa sababu hawakumtii;
watakuwa watu wa kutangatanga
miongoni mwa mataifa.