The chat will start when you send the first message.
1Basi mtu mmoja, jina lake Lazaro, alikuwa mgonjwa. Yeye alikuwa akiishi Bethania, kijiji cha Mariamu na Martha dada yake.
2(Huyu Mariamu, ambaye Lazaro kaka yake alikuwa mgonjwa, ndiye alimpaka Bwana mafuta na kuifuta miguu yake kwa nywele zake.)
3Hivyo hawa dada wawili walituma ujumbe kwa Yesu kumwambia, “Bwana, yule umpendaye ni mgonjwa.”
4Lakini Yesu aliposikia hayo, akasema, “Ugonjwa huu hautaleta mauti, bali ni wa kudhihirisha utukufu wa Mungu, ili Mwana wa Mungu apate kutukuzwa kutokana na ugonjwa huu.”
5Yesu aliwapenda Martha, Mariamu na Lazaro ndugu yao.
6Hata hivyo, baada ya kusikia kwamba Lazaro ni mgonjwa, alikawia huko alikokuwa kwa siku mbili zaidi.
7Ndipo akawaambia wanafunzi wake, “Haya, turudi Yudea.”
8Wanafunzi wake wakamwambia, “Rabi, Wayahudi walikuwa wanataka kukupiga mawe, nawe unataka kurudi huko?”
9Yesu akawajibu, “Si kuna saa kumi na mbili za mchana katika siku moja? Wanaotembea mchana hawawezi kujikwaa, kwa maana wanaona kwa nuru ya ulimwengu huu.
10Lakini wale wanaotembea usiku hujikwaa kwa sababu hawana nuru ndani yao.”
11Baada ya kusema haya, Yesu akawaambia, “Rafiki yetu Lazaro amelala, lakini naenda kumwamsha.”
12Wanafunzi wakamwambia, “Bwana, kama amelala usingizi ataamka.”
13Hata hivyo, Yesu alikuwa anazungumzia kuwa Lazaro amekufa, lakini wanafunzi wake hawakuelewa, walidhani kwamba anasema Lazaro amelala usingizi tu.
14Kwa hiyo Yesu akawaambia waziwazi, “Lazaro amekufa.
15Hata hivyo nafurahi kwa kuwa sikuwako huko kabla ya Lazaro kufa, ili mpate kuamini. Lakini sasa twendeni kwake.”
16Tomaso (aliyeitwa Pacha) akawaambia wanafunzi wenzake, “Sisi nasi twendeni tukafe pamoja naye.”
17Yesu alipowasili huko alikuta Lazaro amekuwa kaburini siku nne.
18Basi Bethania ulikuwa karibu na Yerusalemu, umbali wa yamkini maili mbili,[#11:18 kama kilomita 3]
19na Wayahudi wengi walikuwa wamekuja kuwafariji Martha na Mariamu kwa ajili ya kufiwa na ndugu yao.
20Martha aliposikia kwamba Yesu anakuja, alitoka kwenda kumlaki, ila Mariamu alibaki nyumbani.
21Martha akamwambia Yesu, “Bwana, kama ungekuwa hapa, ndugu yangu hangekufa.
22Lakini sasa ninajua kuwa chochote utakachomwomba Mungu, atakupa.”
23Yesu akamwambia, “Ndugu yako atafufuka.”
24Martha akamjibu, “Ninajua ya kuwa atafufuka wakati wa ufufuo wa wafu siku ya mwisho.”
25Yesu akamwambia, “Mimi ndiye huo ufufuo na uzima. Yeye aniaminiye mimi, hata akifa atakuwa anaishi;
26na yeyote aishiye na kuniamini hatakufa kabisa hata milele. Je, unasadiki haya?”
27Martha akamwambia, “Ndiyo Bwana, ninaamini ya kuwa wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu, yeye ajaye ulimwenguni.”[#11:27 maana yake Masiya , yaani Aliyetiwa mafuta.]
28Baada ya kusema haya, Martha alienda akamwita Mariamu dada yake faraghani na kumwambia, “Mwalimu yuko hapa anakuita.”
29Mariamu aliposikia hivyo, akaondoka upesi, akaenda hadi alipokuwa Yesu.
30Yesu alikuwa hajaingia kijijini, bali alikuwa bado yuko mahali pale alipokutana na Martha.
31Wale Wayahudi waliokuwa pamoja na Mariamu nyumbani wakimfariji walipoona ameondoka haraka na kutoka nje, walimfuata wakidhani kwamba alikuwa anaenda kule kaburini kulilia huko.
32Mariamu alipofika mahali pale Yesu alipokuwa, alipiga magoti miguuni pake na kusema, “Bwana, kama ungekuwa hapa, ndugu yangu hangekufa.”
33Yesu alipomwona Mariamu akilia na wale Wayahudi waliokuja pamoja naye pia wakilia, Yesu alisikia uchungu moyoni, akafadhaika sana.
34Akauliza, “Mmemweka wapi?”
Wakamwambia, “Bwana, njoo upaone.”
35Yesu akalia machozi.
36Ndipo Wayahudi wakasema, “Tazama jinsi alivyompenda Lazaro!”
37Lakini wengine wakasema, “Je, yule aliyefungua macho ya kipofu, hakuweza kumfanya na huyu asife?”
38Yesu akafika penye kaburi akiwa amefadhaika sana kwa mara nyingine. Hilo kaburi lilikuwa pango ambalo jiwe liliwekwa kwenye ingilio lake.
39Yesu akasema, “Liondoeni jiwe.”
Martha dada yake yule aliyekuwa amekufa akasema, “Lakini Bwana, wakati huu atakuwa ananuka kwani amekwisha kuwa kaburini siku nne.”
40Yesu akamwambia, “Sikukuambia kwamba ukiamini utauona utukufu wa Mungu?”
41Kwa hiyo wakaliondoa lile jiwe kutoka kaburini. Yesu akainua macho yake juu, akasema, “Baba, ninakushukuru kwa kuwa wanisikia.
42Ninajua ya kuwa wewe hunisikia siku zote, lakini nimesema haya kwa ajili ya watu hawa waliosimama hapa, ili wapate kuamini ya kuwa wewe umenituma.”
43Baada ya kusema haya, Yesu akapaza sauti yake, akaita, “Lazaro, njoo huku!”
44Yule aliyekuwa amekufa akatoka nje, mikono yake na miguu yake ikiwa imeviringishiwa vitambaa vya kitani na leso usoni pake.
Yesu akawaambia, “Mfungueni; mwacheni aende zake.”
45Hivyo Wayahudi wengi waliokuwa wamekuja kumfariji Mariamu walipoona yale Yesu aliyoyatenda, wakamwamini.
46Lakini baadhi yao wakaenda kwa Mafarisayo na kuwaambia mambo Yesu aliyoyafanya.
47Kwa hiyo viongozi wa makuhani na Mafarisayo wakaita mkutano wa Baraza la Wayahudi.[#11:47 ina maana ya Sanhedrin ambalo lilikuwa baraza la juu kabisa la utawala wa Kiyahudi; liliundwa na wazee 70 pamoja na kuhani mkuu.]
Wakaulizana, “Tufanyeje? Huyu mtu anafanya ishara nyingi.
48Tukimwacha aendelee hivi, kila mtu atamwamini, nao Warumi watakuja na kupaharibu mahali petu patakatifu na taifa letu.”
49Mmoja wao aliyeitwa Kayafa, aliyekuwa kuhani mkuu mwaka huo, akasema, “Ninyi hamjui kitu chochote!
50Hamjui kwamba ni afadhali mtu mmoja afe kwa ajili ya watu, kuliko taifa lote liangamie?”
51Hakusema haya kutokana na mawazo yake mwenyewe, bali kama kuhani mkuu mwaka huo, alitabiri kuwa Yesu angekufa kwa ajili ya taifa la Wayahudi;
52wala si kwa ajili ya taifa hilo pekee, bali pia kwa ajili ya watoto wa Mungu waliotawanyika, ili kuwaleta pamoja na kuwafanya wawe wamoja.
53Hivyo tangu siku hiyo wakawa wanafanya mipango ili wamuue Yesu.
54Kwa hiyo Yesu akawa hatembei tena hadharani miongoni mwa Wayahudi, bali alijitenga akaenda sehemu iliyo karibu na jangwa kwenye kijiji kiitwacho Efraimu. Akakaa huko na wanafunzi wake.
55Basi Pasaka ya Wayahudi ilipokuwa imekaribia, watu wengi walitoka vijijini wakaenda Yerusalemu ili wakajitakase kabla ya Pasaka.
56Watu wakawa wanamtafuta Yesu, nao waliposimama kwenye ua la Hekalu, waliulizana, “Je, mtu huyu hatakuja kamwe kwenye Sikukuu?”
57Viongozi wa makuhani na Mafarisayo walikuwa wametoa amri kuwa yeyote atakayejua mahali Yesu aliko, lazima atoe taarifa ili wapate kumkamata.