The chat will start when you send the first message.
1Taabu gani hii niliyo nayo!
Nimefanana na yule akusanyaye
matunda ya kiangazi,
aokotaye masazo baada ya kuvunwa
shamba la mizabibu;
hakuna kishada chenye matunda ya kula,
hakuna hata ile tini ya mwanzoni ninayoitamani.
2Wanaomcha Mungu wameondolewa kutoka nchi;
hakuna mtu mnyofu hata mmoja aliyebaki.
Watu wote wanavizia kumwaga damu,
kila mmoja anamwinda ndugu yake kwa wavu.
3Mikono yote miwili ni hodari katika kufanya ubaya,
mtawala anadai zawadi,
hakimu anapokea rushwa,
wenye nguvu wanaamuru wanachotaka:
wote wanapanga njama pamoja.
4Aliye mwema kupita wote kati yao
ni kama mchongoma,
anayeonekana mnyofu zaidi miongoni mwao
ni mbaya kuliko uzio wa miiba.
Siku ya walinzi wako imewadia,
siku Mungu atakayokutembelea.
Sasa ni wakati wao
wa kuchanganyikiwa.
5Usimtumaini jirani;
usiweke matumaini kwa rafiki.
Hata kwa yule alalaye kifuani mwako
uwe mwangalifu kwa maneno yako.
6Kwa kuwa mwana humdharau baba yake,
naye binti huinuka dhidi ya mama yake,
mkwe kuwa kinyume na mama mkwe wake:
adui wa mtu ni wale wa nyumbani mwake hasa.
7Lakini mimi, namtazama Bwana kwa matumaini,
namngoja Mungu Mwokozi wangu;
Mungu wangu atanisikia mimi.
8Usifurahie msiba wangu, ee adui yangu!
Ingawa nimeanguka, nitainuka.
Japo ninaketi gizani,
Bwana atakuwa nuru yangu.
9Kwa sababu nimetenda dhambi dhidi yake,
nitabeba ghadhabu ya Bwana ,
hadi atakapotetea shauri langu
na kuithibitisha haki yangu.
Atanileta nje kwenye mwanga,
nami nitaiona haki yake.
10Kisha adui yangu ataliona
naye atafunikwa na aibu,
yule aliyeniambia,
“Yu wapi Bwana Mungu wako?”
Macho yangu yataona kuanguka kwake,
hata sasa atakanyagwa chini ya mguu
kama tope barabarani.
11Siku ya kujenga kuta zako itawadia,
siku ya kupanua mipaka yako.
12Siku hiyo watu watakuja kwako
kutoka Ashuru na miji ya Misri,
hata kutoka Misri hadi Mto Frati,
na kutoka bahari hadi bahari,
na kutoka mlima hadi mlima.
13Dunia itakuwa ukiwa kwa sababu ya wakazi wake,
kwa sababu ya matunda ya matendo yao.
14Wachunge watu wako kwa fimbo yako,
kundi la urithi wako,
ambalo linaishi peke yake msituni,
katika maeneo ya malisho yenye rutuba.
Waache walishe katika Bashani na Gileadi
kama ilivyokuwa siku za kale.
15“Kama siku zile mlipotoka Misri,
nitawaonesha maajabu yangu.”
16Mataifa yataona na kuaibika,
waliondolewa nguvu zao zote.
Wataweka mikono yao kwenye vinywa vyao
na masikio yao yatakuwa na uziwi.
17Wataramba mavumbi kama nyoka,
kama viumbe vinavyotambaa ardhini.
Watatoka nje ya mapango yao wakitetemeka;
watamgeukia Bwana Mungu wetu kwa hofu
nao watakuogopa.
18Ni nani Mungu kama wewe,
ambaye anaachilia dhambi
na kusamehe makosa
ya mabaki ya urithi wake?
Wewe huwi na hasira milele,
bali unafurahia kuonesha rehema.
19Utatuhurumia tena,
utazikanyaga dhambi zetu
chini ya nyayo zako,
na kutupa maovu yetu yote
katika vilindi vya bahari.
20Utakuwa wa kweli kwa Yakobo,
nawe utamwonesha Abrahamu rehema,
kama ulivyowaahidi kwa kiapo baba zetu
siku za kale.