Mithali 23

Mithali 23

1Uketipo kula chakula na mtawala,

angalia vyema kile kilicho mbele yako,

2na utie kisu kooni mwako

kama ukiwa mlafi.

3Usitamani vyakula vyake vitamu

kwa kuwa chakula hicho ni cha hila.

4Usijitaabishe ili kuupata utajiri,

uwe na hekima kuonesha kujizuia.

5Kufumba na kufumbua utajiri hutoweka,

huwa kama umepata mabawa ghafula,

ukaruka na kutoweka angani kama tai.

6Usile chakula cha mtu mchoyo,

usitamani vyakula vyake vitamu,

7kwa maana yeye ni aina ya mtu

ambaye kila mara anafikiri kuhusu gharama.

Anakuambia, “Kula na kunywa,”

lakini moyo wake hauko pamoja nawe.

8Utatapika kile kidogo ulichokula,

nawe utakuwa umepoteza bure

maneno yako ya kumsifu.

9Usizungumze na mpumbavu,

kwa maana atadhihaki hekima ya maneno yako.

10Usisogeze jiwe la mpaka wa zamani

wala kunyemelea kwenye mashamba ya yatima,

11kwa kuwa Mtetezi wao ni mwenye nguvu,

atawatetea dhidi yako.

12Elekeza moyo wako kwenye mafundisho

na masikio yako kwenye maneno ya maarifa.

13Usimnyime mtoto adhabu,

ukimwadhibu kwa fimbo, hatakufa.

14Mwadhibu kwa fimbo

na kuiokoa nafsi yake kutoka mautini.

15Mwanangu, kama moyo wako una hekima,

basi moyo wangu utafurahi,

16utu wangu wa ndani utafurahi,

wakati midomo yako

itakapozungumza lililo sawa.

17Usiuruhusu moyo wako kuwaonea wivu wenye dhambi,

bali kila mara uwe na bidii katika kumcha Bwana .

18Hakika kuna tumaini la baadaye kwa ajili yako,

nalo tarajio lako halitakatiliwa mbali.

19Sikiliza, mwanangu na uwe na hekima,

weka moyo wako kwenye njia iliyo sawa.

20Usiwe miongoni mwa wanywao mvinyo,

au wale walao nyama kwa pupa,

21kwa maana walevi na walafi huwa maskini,

nako kusinzia huwavika matambara.

22Msikilize baba yako, aliyekuzaa,

wala usimdharau mama yako atakapokuwa mzee.

23Nunua kweli wala usiiuze,

pata hekima, adabu na ufahamu.

24Baba wa mwenye haki ana furaha kubwa,

naye aliye na mwana mwenye hekima humfurahia.

25Baba yako na mama yako na wafurahi,

mama aliyekuzaa na ashangilie!

26Mwanangu, nipe moyo wako,

macho yako na yafuate njia zangu,

27kwa maana kahaba ni shimo refu

na mwanamke mpotovu ni kisima chembamba.

28Kama mnyangʼanyi, hungojea akivizia,

naye huzidisha wasio waaminifu miongoni mwa wanaume.

29Ni nani mwenye ole?

Ni nani mwenye huzuni?

Ni nani mwenye ugomvi?

Ni nani mwenye malalamiko?

Ni nani aliye na majeraha yasiyo na sababu?

Ni nani mwenye macho mekundu?

30Ni hao wanaokaa sana kwenye mvinyo,

hao wanaoenda kuonja mabakuli ya mvinyo uliochanganywa.

31Usiukodolee macho mvinyo ukiwa mwekundu,

unapometameta kwenye bilauri,

unaposhuka taratibu!

32Mwishowe huuma kama nyoka

na kutia sumu yake kama nyoka mwenye sumu.

33Macho yako yataona mambo mageni,

na moyo wako kuwazia mambo yaliyopotoka.

34Utakuwa kama alalaye baharini,

alalaye juu ya kamba ya merikebu.

35Utasema, “Wamenipiga lakini sikuumia!

Wamenichapa, lakini sisikii!

Nitaamka lini

ili nikanywe tena?”

Neno: Biblia Takatifu™ Neno™ Hakimiliki © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 na Biblica, Inc. Imetumiwa kwa ruhusa. Haki zote zimehifadhiwa duniani kote. Kiswahili Contemporary Version™ Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 by Biblica, Inc. Used with permission. All rights reserved worldwide.
Published by: Biblica, Inc.