Mithali 9

Mithali 9

Makaribisho ya hekima na ya upumbavu

1Hekima amejenga nyumba yake;

amechonga nguzo zake saba.

2Ameandaa nyama na kuchanganya divai yake;

pia ameandaa meza yake.

3Amewatuma wajakazi wake, naye huita

kutoka mahali pa juu sana pa mji.

4Anawaambia wale wasio na akili,

“Wote ambao ni wajinga na waje hapa!

5Njooni, mle chakula changu

na mnywe divai niliyoichanganya.

6Acheni njia zenu za ujinga nanyi mtaishi;

tembeeni katika njia ya ufahamu.

7“Yeyote anayemkosoa mwenye dhihaka

hukaribisha matusi;

yeyote anayekemea mtu mwovu

hupatwa na matusi.

8Usimkemee mwenye dhihaka, la sivyo atakuchukia;

mkemee mwenye hekima naye atakupenda.

9Mfundishe mtu mwenye hekima

naye atakuwa na hekima zaidi;

mfundishe mtu mwadilifu

naye atazidi kufundishika.

10“Kumcha Bwana ndicho chanzo cha hekima,

na kumjua Aliye Mtakatifu ni ufahamu.

11Kwa maana kwa msaada wangu

siku zako zitakuwa nyingi,

na miaka itaongezwa katika maisha yako.

12Kama wewe una hekima, hekima yako itakupa tuzo;

kama wewe ni mtu wa mzaha,

wewe mwenyewe ndiwe utateseka.”

13Mwanamke aitwaye Mpumbavu ana kelele;

hana adabu na hana maarifa.

14Huketi kwenye mlango wa nyumba yake,

kwenye kiti katika mahali pa juu sana pa mji,

15akiita wale wanaopita karibu,

wanaoenda moja kwa moja kwenye njia yao.

16Anawaambia wale wasio na akili,

“Wote ambao ni wajinga na waje hapa ndani!

17Maji yaliyoibiwa ni matamu;

chakula kinacholiwa sirini ni kitamu!”

18Lakini hawajui hata kidogo kuwa wafu wako humo,

kwamba wageni wake huyo mwanamke

wako katika vilindi vya Kuzimu.

Neno: Biblia Takatifu™ Neno™ Hakimiliki © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 na Biblica, Inc. Imetumiwa kwa ruhusa. Haki zote zimehifadhiwa duniani kote. Kiswahili Contemporary Version™ Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 by Biblica, Inc. Used with permission. All rights reserved worldwide.
Published by: Biblica, Inc.