The chat will start when you send the first message.
1Kisha Yakobo akawaita wanawe, akawaambia: Kusanyikeni, niwaeleze, yatakayowapata siku za sasa zitakapokwisha!
2Kusanyikeni, wana wa Yakobo, msikilize!
Msikilizeni baba yenu Isiraeli!
3Wewe Rubeni, u mwana wa kwanza,
u nguvu yangu na uwezo wangu wa kwanza,
ukuu wako hutukuzwa, ukuu wako ni wa nguvu.
4Lakini kwa kububujika kama maji hutapata ukuu wa kweli,
kwani ulipokipanda kitanda cha baba yako,
ndipo, ulipoyachafua malalo yangu kwa kuyapandia.
5Simeoni na Lawi ni ndugu kweli,
panga zao ni vyombo vya ukorofi.
6Roho yangu isiingie penye njama yao,
wala moyo wangu usifanye bia na mikutano yao!
Kwani kwa makali yao waliua watu,
kwa majivuno yao wakakata madume ya ng'ombe mishipa.
7Na yaapizwe makali yao kwa kuwa yenye nguvu!
Na yaapizwe machafuko yao kwa kuwa yenye upingani!
Na niwagawanye kwao Wayakobo,
na niwatawanye kwao Waisiraeli!
8Wewe Yuda, ndugu zako watakusifu;
mkono wako utawakamata wachukivu wako penye kosi,
nao wana wa baba yako watakuangukia.
9Yuda ni mwana simba.
Mwanangu, ulipokwisha kukamata, hupanda kupumzika
na kulala kama simba au kama mamake simba;
yuko nani atakayekuamsha?
10Bakora ya kifalme haitaondoka kwake Yuda,
wala fimbo la mwenye amri halitaondoka miguuni pake,
mpaka atakapokuja mwenye kutuliza,
ambaye makabila ya watu watamtii.
11Kipunda chake hukifunga mizabibuni,
naye mwana punda humlisha miche ya mizabibu mizuri,
huyafua mavazi yake katika mvinyo,
nazo nguo zake katika damu za zabibu.
12Macho yake huwa mekundu kwa kunywa mvinyo,
nayo meno yake huwa meupe kwa kunywa maziwa.
13Zebuluni atakaa pwani, Bahari Kubwa iliko,
huko pwani, merikebu zinakofikia, apakane nao Wasidoni.
14Isakari ni punda mwenye mifupa migumu,
hupenda kulala, katikati ya mazizi ya kondoo.
15Atakapoona matuo kuwa mema,
atakapoiona nayo nchi hii kuwa ya kumpendeza,
ndipo, atakapouinamisha mgongo wake kuchukua mizigo,
awe mtumishi wa kufanya kazi za nguvu.
16Dani atawaamua walio watu wake
akiwa kama wenzake walio mashina ya Isiraeli.
17Dani atakuwa nyoka njiani, atakuwa piri penye mikondo,
awaume farasi visigino, waliowapanda waanguke nyuma.
18Ninaungojea wokovu wako, Bwana![#Sh. 119:166; Hab. 2:3.]
19Gadi atashambuliwa na vikosi vya vita,
lakini naye atawashambulia na kuwanyatia.
20Kwake Aseri ndiko, vyakula vya manono vitakakotoka,
naye ndiye atakayewapatia wafalme vyakula vya urembo.
21Nafutali ni kulungu aliyefunguliwa kukimbia,
huimba nyimbo zilizo nzuri zaidi.
22Yosefu ni tawi la mti wa matunda,
tawi la mti wa matunda ulioko kwenye mboji,
kwa hiyo matawi yake hutambaa na kuufunika ukuta.
23Ijapo wapiga mishale wamchokoze kwa kumgombeza
24na kumchukia, upindi wake hushupaa vivyo hivyo,
nazo nguvu za mikono yake ziko tayari vivyo hivyo, yumo
mikoni mwake amtawalaye Yakobo,
hushikwa na mchungaji aliye mwamba wa Isiraeli.
25Mungu wa baba yako ndiye atakayekusaidia
Mwenyezi Mungu ndiye atakayekubariki
kwa mbaraka zitokazo mbinguni juu
na kwa mbaraka zitokazo vilindini ndani ya nchi
na kwa mbaraka zitokazo maziwani na tumboni.
26Mbaraka za baba yako zina nguvu
kuzishinda mbaraka zao walionizaa,
zitakupendeza kuliko matunu ya vilima vya kale na kale.
Hizo ndizo zitakazokijia kichwa chake Yosefu,
nao utosi wake yeye aliyewekwa kwa
kutengwa na ndugu zake.
27Benyamini ni mbwa wa mwitu mwenye uchu wa damu,
asubuhi hula mawindo, jioni hugawanya mateka.
28Haya ndiyo mashina yote kumi na mawili ya Isiraeli, nayo haya ndiyo yote, baba yao aliyowaambia alipowabariki, naye aliwabariki na kumpa kila mmoja mbaraka yake yeye.
29Kisha akawaagiza na kuwaambia: Mimi sasa nitakapochukuliwa kwenda kwao walio ukoo wangu, sharti mnizike kwa baba zangu katika lile pango, lililoko shambani kwake Mhiti Efuroni![#1 Mose 23:16-20; 47:30.]
30Ndilo pango lile lililoko shambani kwa Makipela kuelekea Mamure; shamba hilo Aburahamu alilinunua kwa Mhiti Efuroni kuwa mahali pake yeye pa kuzikia.
31Mle pangoni ndimo, walimomzika Aburahamu na mkewe Sara, naye Isaka na mkewe Rebeka waliwazika humo, naye Lea nilimzika humo.[#1 Mose 25:9; 35:29.]
32Ndilo lile shamba lililonunuliwa kwa wana wa Hiti pamoja na lile pango lililoko.
33Yakobo alipokwisha kuwaagiza wanawe maneno haya akaikunja miguu yake kitandani, akazimia, akachukuliwa kwenda kwao walio wa ukoo wake.