2 Mambo ya Nyakati 10

2 Mambo ya Nyakati 10

Uasi juu ya Rehoboamu

1Rehoboamu akaenda Shekemu; maana Israeli wote walikuwa wamekuja Shekemu, ili wamfanye mfalme.[#1 Fal 12:11]

2Ikawa Yeroboamu mwana wa Nebati aliposikia tendo hilo (maana alikuwa Misri, alikokwenda alipomkimbia mfalme Sulemani) Yeroboamu akarudi kutoka Misri.[#1 Fal 11:40]

3Wakatuma ujumbe, wakamwita, Yeroboamu akaja na Israeli wote, wakamwambia Rehoboamu, wakasema,

4Baba yako alilifanya zito kongwa letu; basi sasa upunguze utumwa mgumu wa baba yako, na kongwa lake zito alilotutwika, nasi tutakutumikia.[#1 Sam 8:11-18; 1 Fal 4:7; 5:15; 9:15; Mt 11:29,30; 23:4; 1 Yoh 5:3]

5Akawaambia, Mnirudie baada ya siku tatu. Watu wakaenda zao.

6Mfalme Rehoboamu akataka shauri kwa wazee, waliosimama mbele ya Sulemani baba yake, alipokuwa hai bado, akasema, Mnanipa shauri gani la kuwajibu watu hawa?[#Ayu 8:8,9; 32:7]

7Wakamwambia, wakasema, Ukiwa mwema kwao watu hawa, na kuwapendeza, na kuwaambia maneno mazuri, hapo watakuwa watumishi wako siku zote.[#1 Fal 12:7; Neh 5:19; Zab 112:5; Mit 15:1]

8Lakini akaliacha shauri lile la wazee walilompa, akataka shauri kwa wale vijana wa rika yake, waliokuwa washauri wake.[#2 Sam 17:14; 2 Nya 25:16; Mit 1:25; 13:20; Mhu 10:2]

9Akawaambia, Je! Mwanipa shauri gani la kuwajibu watu hawa, waliosema nami, wakisema, kongwa alilotutwika baba yako utufanyie liwe jepesi.

10Na wale vijana waliokua pamoja naye wakamwambia, wakasema, Uwaambie hivi watu wale waliosema nawe, wakinena, Baba yako alilifanya kongwa letu kuwa zito, lakini wewe tufanyie jepesi; uwaambie hivi, Kidole changu cha mwisho ni kinene kuliko kiuno cha baba yangu.

11Basi kama baba yangu aliwatwika kongwa zito, mimi nitaongeza kongwa lenu; baba yangu aliwapiga kwa mijeledi, lakini mimi nitawapiga kwa nge.

12Basi Yeroboamu na watu wote wakamjia Rehoboamu siku ya tatu, kama mfalme alivyoamuru, akisema, Mnirudie siku ya tatu.

13Mfalme akawajibu kwa ukali; mfalme Rehoboamu akaliacha shauri la wazee, akasema nao kwa shauri la vijana,[#Mit 12:13; 14:16]

14akinena, Baba yangu aliwafanyia kongwa zito, nami nitawaongezea; baba yangu aliwapiga kwa mijeledi, lakini mimi nitawapiga kwa nge.

15Basi mfalme hakuwasikia watu wale; maana jambo hili lilitoka kwa Mungu, ili alithibitishe neno lake alilomwambia Yeroboamu mwana wa Nebati kwa mkono wa Ahiya Mshiloni.[#Mwa 50:20; 1 Sam 2:25; 1 Fal 12:15,24; Amo 3:6; 1 Fal 11:29]

16Basi Israeli wote walipoona ya kuwa mfalme hawasikilizi, watu wakamjibu mfalme, wakasema, Tuna sehemu gani katika Daudi? Wala hatuna urithi katika mwana wa Yese; kila mtu aende zake hemani, enyi Israeli, sasa itunze nyumba yako mwenyewe ewe Daudi. Basi wakaenda zao Israeli wote hemani kwao.

17Lakini kuhusu wana wa Israeli waliokaa katika miji ya Yuda, Rehoboamu alitawala juu yao.

18Ndipo mfalme Rehoboamu akamtuma Adoramu, msimamizi wa shokoa; nao wana wa Israeli wakampiga kwa mawe hadi akafa. Mfalme Rehoboamu akafanya haraka kupanda garini mwake, ili akimbilie Yerusalemu.

19Hivyo Israeli wakaasi juu ya nyumba ya Daudi, hata leo.[#1 Fal 12:19; 2 Fal 17:21-23; 2 Nya 13:5-7; Mhu 2:19]

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya