The chat will start when you send the first message.
1Katika mwaka wa pili wa utawala wa Artashasta, mfalme mkuu, siku ya kwanza ya mwezi wa Nisani, Mordekai, mwana wa Yairo, mwana wa Semaya, mwana wa Kiseo, wa kabila ya Benyamini, aliota ndoto. Huyu Mordekai alikuwa Myahudi akikaa katika mji wa Susa, mtu mkuu, mtumishi katika behewa la mfalme. Alikuwa amechukuliwa mateka, wakati Nebukadreza, mfalme wa Babeli, alipomhamisha Yekonia, mfalme wa Uyahudi, kutoka Yerusalemu. Nayo ndoto yake ilikuwa hivi: Tazama! Kelele na ghasia; ngurumo na tetemeko la ardhi; msukosuko juu ya dunia. Na tazama! Kumetokea majoka makubwa mawili, wote wawili tayari kupigana. Mlio wao ulikuwa mkubwa mno, hata kwa kusikia tu mataifa yote walijipanga tayari kwa vita ili kupigana na taifa lenye haki. Na tazama! Siku ya giza na weusi; dhiki na taabu; misiba na wasiwasi mwingi juu ya dunia. Taifa zima la wenye haki wakafadhaika kwa kuogopa mabaya yanayowajia, wakajiweka tayari kufa. Wakamlilia Mungu, hata katika kilio chao, kama katika chemchemi ndogo, kulitokea mto kubwa, maji mengi sana. Nuru ikaangaa, na jua likachomoza; wanyonge wakakwezwa wakawameza wenye fahari. Naye Mordekai alipokwisha kuiota ndoto hiyo ya mambo yaliyokusudiwa na Mungu aliamka; akaihifadhi moyoni mwake, akaitafakari maana yake hata usiku.[#2 Fal 24:10-16]
1Basi, Mordekai alikuwa akipumzika behewani, kama kawaida yake, pamoja na Gabatha na Thara, matowashi wawili wa mfalme waliokuwa walinzi wa behewa. Akasikia mazungumzo yao, akayapeleleza mashauri yao, akapata kufahamu ya kuwa wamejiweka tayari kumshika mfalme Artashasta. Akamwarifu mfalme habari zao. Mfalme akawahoji wale matowashi wawili, nao wakakiri, wakapelekwa kuuawa. Mfalme akayaandikisha mambo hayo kuwa ukumbusho, naye Mordekai pia aliandika habari zake. Mfalme akamwagiza Mordekai atumike behewani, akamtunukia kwa kazi zake. Ikawa Hamani mwana wa Hamedatha, Mbugaya, mtu mwenye heshima kuu kwa mfalme alikuwa ikiwatafuta mabaya Mordekai na watu wake kwa sababu ya hao matowashi wawili wa mfalme.