Kutoka 16

Kutoka 16

Mkate kutoka mbinguni

1Kisha wakasafiri kutoka Elimu, na mkutano wote wa wana wa Israeli wakafikia jangwa la Sini, lililoko kati ya Elimu na Sinai, siku ya kumi na tano ya mwezi wa pili baada ya kutoka kwao nchi ya Misri.[#Eze 30:15]

2Na mkutano mzima wa wana wa Israeli ukawanung'unikia Musa na Haruni, huko barani;[#Kut 15:24; Zab 106:25; 1 Kor 10:10]

3wana wa Israeli wakawaambia, Laiti tungalikufa kwa mkono wa BWANA katika nchi ya Misri, hapo tulipoketi karibu na zile sufuria za nyama, tulipokula vyakula hata kushiba; kwani mmetutoa huko na kututia katika bara hii, ili kutuua kwa njaa kusanyiko hili lote.[#Hes 11:4]

4Ndipo BWANA akamwambia Musa, Tazama, mimi nitawanyeshea ninyi mvua ya mkate kutoka mbinguni; na hao watu watatoka nje na kuokota kila siku sehemu ya siku; ili nipate kuwajaribu, kwamba watakwenda katika sheria yangu, ama sivyo.[#Yn 6:31; Zab 78:24; 105:40; 1 Kor 10:3; Mit 30:8; Mt 6:11; Kum 8:2]

5Kisha itakuwa siku ya sita, ya kwamba watayaandaa hayo watakayoleta ndani, nayo yatakuwa ni mara mbili kuliko wayaokotayo kila siku.[#Law 25:21]

6Musa na Haruni wakawaambia wana wote wa Israeli, Jioni ndipo mtakapojua ya kuwa BWANA amewaleta kutoka nchi ya Misri;[#Kut 6:7; Hes 16:28]

7na asubuhi ndipo mtakapouona utukufu wa BWANA; kwa kuwa yeye husikia manung'uniko yenu mliyomnung'unikia BWANA; na sisi tu nani, hata mkatunung'unikia?[#Isa 35:2; 40:5; Yn 11:4,40]

8Musa akasema, Ndilo litakalokuwa, hapo BWANA atakapowapa nyama wakati wa jioni mle, na asubuhi mikate hata mkakinai; kwa kuwa BWANA asikia manung'uniko yenu mliyomnung'unikia yeye; na sisi tu nani? Manung'uniko yenu hayakuwa juu yetu sisi, ila juu ya BWANA.[#1 Sam 8:7; Lk 10:16; Rum 13:2; 1 The 4:8]

9Musa akamwambia Haruni, Haya, sema na mkutano wote wa wana wa Israeli, Njoni karibu mbele ya BWANA; kwa kuwa yeye ameyasikia manung'uniko yenu.

10Ilikuwa Haruni aliponena na huo mkutano wote wa wana wa Israeli, wakaangalia upande wa bara, na tazama, utukufu wa BWANA ukaonekana katika hilo wingu.[#1 Fal 8:10]

11BWANA akasema na Musa, akinena,

12Nimeyasikia manung'uniko ya wana wa Israeli; haya sema nao ukinena, Wakati wa jioni mtakula nyama, na wakati wa asubuhi mtashiba mkate; nanyi mtajua ya kuwa mimi ndimi BWANA, Mungu wenu.[#Hes 14:27; Kut 6:7; 1 Fal 20:28; Yoe 3:17]

13Ikawa wakati wa jioni, kware wakaja, wakaifunikiza kambi; na wakati wa asubuhi umande ulikuwa juu ya nchi pande zote za kituo.[#Hes 11:31; Zab 78:27,28; Hes 11:9]

14Na ulipokauka ule umande uliokuwa juu ya nchi, kumbe! Juu ya uso wa bara kitu kidogo kilichoviringana, kidogo kama barafu juu ya nchi.[#Hes 11:7; Kum 8:3; Neh 9:15; Zab 78:24; 105:40]

15Wana wa Israeli walipokiona, wakaambiana, Nini hiki? Maana hawakujua ni kitu gani. Musa akawaambia, Ndio mkate ambao BWANA amewapa ninyi, mle.[#1 Kor 10:3; Isa 25:6; Yn 6:31,49,58]

16Neno hili ndilo aliloagiza BWANA, Okoteni ninyi kitu hicho kila mtu kama ulaji wake ulivyo; kila mtu pishi moja kama hesabu ya watu wenu ilivyo; ndivyo mtakavyotwaa, kila mtu kwa ajili ya hao walioko hemani mwake.[#Kut 16:36; #16:16 Katika Kiebrania ni Omeri.]

17Wana wa Israeli wakafanya hivyo, wakaokota wengine zaidi, wengine kupungua.

18Nao walipoipima kwa pishi, yeye aliyekuwa ameokota kingi hakubakiwa na kitu, na yeye aliyekuwa ameokota kichache hakupungukiwa; wakaokota kila mtu kama ulaji wake ulivyokuwa.[#2 Kor 8:15]

19Musa akawaambia, Mtu awaye yote asikisaze hata asubuhi.

20Lakini hawakumsikiza Musa; wengine miongoni mwao wakakisaza hata asubuhi, nacho kikaingia mabuu na kutoa uvundo; Musa akawakasirikia sana.

21Basi wakaokota asubuhi baada ya asubuhi, kila mtu kama ulaji wake ulivyokuwa; na hapo jua lilipokuwa ni kali, kikayeyuka.

22Basi ikawa siku ya sita wakaokota kile chakula sehemu maradufu, kila mtu pishi mbili; na wazee wote wa mkutano wakaenda na kumwambia Musa.

23Akawaambia, Ndilo neno alilonena BWANA Kesho ni starehe takatifu, Sabato takatifu kwa BWANA; okeni mtakachooka, na kutokosa mtakachotokosa; na hicho kitakachowasalia jiwekeeni kilindwe hata asubuhi.[#Kut 20:8; 31:15; 35:3; Mwa 2:3; Law 23:3]

24Basi wakakiweka hata asubuhi, kama Musa alivyowaagiza; nacho hakikutoa uvundo wala kuingia mabuu.[#Kut 16:20]

25Musa akasema, Haya, kuleni hiki leo; kwa kuwa leo ni Sabato ya BWANA; leo hamtakiona nje barani.[#Ebr 4:4; Mt 12:12; 24:20]

26Siku sita mtaokota; lakini siku ya saba ni Sabato, siku hiyo hakitapatikana.[#Kut 20:9,10]

27Ikawa siku ya saba wengine wakatoka kwenda kukiokota, wasikione.

28BWANA akamwambia Musa, Mtakataa kuyashika maagizo yangu na sheria zangu hata lini?[#2 Fal 17:14; Zab 78:10,22; 106:13; Yer 4:14]

29Angalieni, kwa kuwa BWANA amewapa ninyi hiyo Sabato, kwa sababu hii huwapa siku ya sita chakula cha siku mbili; kaeni kila mtu mahali pake, mtu awaye yote asiondoke mahali pake kwa siku ya saba.

30Basi hao watu wakapumzika kwa siku ya saba.

31Na nyumba ya Israeli wakakiita jina lake Mana; nacho kilikuwa mfano wa chembe za mtama, nyeupe; na utamu wake ulikuwa kama utamu wa maandazi membamba yaliyoandaliwa kwa asali.[#Hes 11:7-8]

32Musa akasema, Hili ni neno BWANA aliloliamuru, Pishi moja ya kitu hicho na kiwekwe kwa ajili ya vizazi vyenu; ili kwamba wao wapate kukiona kile chakula nilichowalisha ninyi barani, hapo nilipowaleta kutoka nchi ya Misri.

33Basi Musa akamwambia Haruni, Twaa kopo, ukatie pishi moja ya hiyo Mana ndani yake, uiweke mbele ya BWANA, ilindwe kwa ajili ya vizazi vyenu.[#Ebr 9:4]

34Kama vile BWANA alivyomwagizia Musa ndivyo Haruni alivyoiweka hapo mbele ya Ushahidi, ili ilindwe.[#Kut 25:16,21; 40:20; Hes 17:10; Kum 10:5; 1 Fal 8:9]

35Na wana wa Israeli walikula Mana muda wa miaka arubaini, hata walipofikia nchi iliyo na watu, wakala ile Mana, hata walipofikia mipakani mwa nchi ya Kanaani.[#Yos 5:12; Hes 33:38; Kum 8:2,3; Neh 9:20,21; Yn 6:31,49]

36Hiyo omeri ni sehemu kumi ya efa.

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya