Isaya 45

Isaya 45

Koreshi, chombo cha Mungu

1Haya ndiyo BWANA amwambiayo Koreshi, masihi wake, ambaye nimemshika mkono wake wa kulia, ili kutiisha mataifa mbele yake, nami nitalegeza nguvu za wafalme; ili kufungua milango mbele yake, hata malango hayatafungwa.[#Zab 73:23; Isa 41:13; #45:1 Au, mtiwa mafuta (tazama 1 Sam 2:10).; #45:1 Katika Kiebrania ni: Nitalegeza viuno vya wafalme.]

2Nitakwenda mbele yako, na kupasawazisha mahali palipoparuza; nitavunja vipande vipande milango ya shaba, na kukatakata mapingo ya chuma;

3nami nitakupa hazina za gizani, na mali zilizofichwa za mahali pa siri, upate kujua ya kuwa mimi ni BWANA, nikuitaye kwa jina lako, naam, Mungu wa Israeli.[#Kut 33:12]

4Kwa ajili ya Yakobo, mtumishi wangu, na Israeli, mteule wangu, nimekuita kwa jina lako; nimekupa jina la sifa; ijapokuwa hukunijua.[#Isa 44:1; Mdo 17:23; Gal 1:8,9; Efe 2:12; 1 The 4:5]

5Mimi ni BWANA, wala hapana mwingine; zaidi yangu mimi hapana Mungu; nitakuimarisha ijapokuwa hukunijua;[#Kum 4:35; Zab 18:32; #45:5 Katika Kiebrania ni: kufunga mshipi.]

6ili wapate kujua toka maawio ya jua, na toka magharibi, ya kuwa hapana mwingine zaidi ya mimi; Mimi ni BWANA, wala hapana mwingine.[#Zab 102:15; Mal 1:11]

7Mimi naiumba nuru, na kulihuluku giza; mimi nafanya suluhu, na kuhuluku ubaya; Mimi ni BWANA, niyatendaye hayo yote.[#Amo 3:6]

8Dondokeni, enyi mbingu, toka juu,[#Zab 85:11]

Mawingu na yamwage haki;

Nchi na ifunuke, ili kutoa wokovu,

Nayo itoe haki ikamee pamoja;

Mimi, BWANA, nimeiumba.

9Ole wake ashindanaye na Muumba wake! Kigae kimoja katika vigae vya dunia! Je! Udongo umwambie yeye aufinyangaye; Unatengeneza nini? Au chombo ulichotengeneza hakina mikono?[#Rum 9:20; Isa 64:8; Yer 18:6]

10Ole wake amwambiaye baba yake, Wazaa nini? Au mwanamke, Una uchungu wa kujifungua nini?

11BWANA, Mtakatifu wa Israeli, na Muumba wake, asema hivi; Niulize habari za mambo yatakayokuja; mambo ya wana wangu, na habari ya kazi ya mikono yangu; haya! Niagizeni.[#Yer 31:9; Isa 29:23]

12Mimi nimeiumba dunia, nimemhuluku mwanadamu juu yake; Mimi, naam, mikono yangu mimi, imezitanda mbingu, na jeshi lake lote nimeliamuru.[#Yer 27:5]

13Mimi nimemwinua katika haki, nami nitazinyosha njia zake zote; ataujenga mji wangu, naye atawaacha huru watu wangu waliohamishwa, si kwa kulipwa fedha, wala kwa kupewa zawadi, asema BWANA wa majeshi.[#Ezr 1:1; Rum 3:24]

14BWANA asema hivi, Kazi ya Misri, na bidhaa ya Kushi, na Waseba, watu walio warefu, watakujia, nao watakuwa wako; watakufuata; watakuja katika minyororo; wataanguka chini mbele yako, watakuomba, wakisema, Hakika Mungu yu ndani yako; wala hapana mwingine, hapana Mungu tena.[#Zab 68:31; Isa 49:23; Zek 8:22; 1 Kor 14:25]

15Hakika wewe u Mungu ujifichaye nafsi yako, Ee Mungu wa Israeli, Mwokozi.[#Kum 29:29; Zab 36:6; Isa 8:17; Rum 11:33]

16Watatahayarika, naam, watafadhaika, wote pia; wale watengenezao sanamu wataingia fadhaa pamoja.

17Bali Israeli wataokolewa na BWANA kwa wokovu wa milele; ninyi hamtatahayarika, wala kufadhaika, milele na milele.[#2 Sam 23:5; Zab 103:17; Hos 1:7; Rum 11:26]

18Maana BWANA, aliyeziumba mbingu, asema hivi; Yeye ni Mungu; ndiye aliyeiumba dunia na kuifanya; ndiye aliyeifanya imara; hakuiumba iwe ukiwa, aliiumba ili ikaliwe na watu; Mimi ni BWANA, wala hapana mwingine.

19Sikusema kwa siri, katika mahali pa nchi ya giza; sikuwaambia wazao wa Yakobo; Nitafuteni bure; Mimi, BWANA, nasema ukweli; nanena mambo ya haki.[#Kum 30:11; Neh 9:13; Zab 19:8; Rum 7:12]

Miungu haiwezi kuokoa Babeli

20Jikusanyeni mje; na kukaribia pamoja, ninyi wa mataifa mliookoka; hawana maarifa wale wachukuao mti wa sanamu yao ya kuchonga; wamwombao mungu asiyeweza kuokoa.[#Yer 44:28; Rum 1:22]

21Hubirini, toeni habari; naam, na wafanye mashauri pamoja; ni nani aliyeonesha haya tangu zamani za kale? Ni nani aliyeyahubiri hapo zamani? Si mimi, BWANA? Wala hapana Mungu zaidi ya mimi; Mungu mwenye haki, mwokozi; hapana mwingine zaidi ya mimi.

22Niangalieni mimi, mkaokolewe, enyi ncha zote za dunia; maana mimi ni Mungu; hapana mwingine.

23Kwa nafsi yangu nimeapa, neno hili limetoka kinywani mwangu katika haki, wala halitarudi, ya kwamba mbele zangu kila goti litapigwa, kila ulimi utaapa.[#Mwa 22:16; Yer 22:5; Ebr 6:13; Mwa 31:53; Kum 6:13; Zab 63:11; Rum 14:11; Flp 2:10-11]

24Mmoja ataniambia, Kwa BWANA, peke yake, iko haki na nguvu; naam, watu watamwendea yeye, na wote waliomkasirikia watatahayarika.

25Katika BWANA wazao wote wa Israeli watapewa haki, na kutukuka.

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya