The chat will start when you send the first message.
1Neno hili ndilo lililomjia Yeremia, kutoka kwa BWANA, kusema,
2Yasikieni maneno ya maagano haya; ukaseme na watu wa Yuda, na wenyeji wa Yerusalemu;
3ukawaambie, BWANA, Mungu wa Israeli, asema hivi, Na alaaniwe mtu asiyeyasikia maneno ya maagano haya,[#Kum 27:26; 28:15; Gal 3:10]
4Niliyowaamuru baba zenu, siku ile nilipowatoa katika nchi ya Misri, katika tanuri ya chuma, nikisema, Itiini sauti yangu, mkafanye sawasawa na yote niwaagizayo ninyi; ndivyo mtakavyokuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wenu;[#Law 26:3]
5ili nipate kukitimiza kiapo nilichowaapia baba zenu, kuwapa nchi itiririkayo maziwa na asali, kama ilivyo hivi leo. Ndipo nikajibu, nikasema, Amina, Ee BWANA.[#Kum 7:12; Zab 105:9]
6Naye BWANA akaniambia, Hubiri maneno haya yote katika miji ya Yuda, na katika njia kuu za Yerusalemu, ukisema, Yasikieni maneno ya maagano haya, mkayafanye.[#Yn 13:17; Rum 2:13]
7Kwa maana niliwashuhudia sana baba zenu, siku ile nilipowatoa katika nchi ya Misri, hata leo, nikiamka mapema na kuwashuhudia, nikisema, Itiini sauti yangu.
8Lakini hawakutii, wala kutega masikio yao, bali walikwenda kila mtu katika ushupavu wa moyo wake mbaya; kwa hiyo nimeleta juu yao maneno yote ya maagano haya, niliyowaamuru wayafanye; lakini hawakuyafanya.
9Naye BWANA akaniambia, Fitina imeonekana katika watu wa Yuda, na katika wenyeji wa Yerusalemu.[#Eze 22:25; Hos 6:9]
10Wameyarudia maovu ya baba zao, waliokataa kusikia maneno yangu; wamewafuata miungu mingine na kuwatumikia; nyumba ya Israeli, na nyumba ya Yuda, wameyavunja maagano yangu niliyoyafanya na baba zao.[#Amu 2:11; Eze 20:18]
11Basi, BWANA asema hivi, Tazama, nitaleta mabaya juu yao, ambayo hawataweza kuyakimbia; nao watanililia, lakini sitawasikiliza.[#Zab 18:41; Mit 1:28; Isa 1:15; Yer 14:12; Mik 3:4; Zek 7:13]
12Ndipo miji ya Yuda, na wenyeji wa Yerusalemu, watakwenda na kuwalilia miungu wawafukiziao uvumba; lakini hawatawaokoa hata kidogo wakati wa taabu yao.[#Kum 32:37; Isa 45:20; 2 Nya 28:22,23]
13Maana hesabu ya miungu yako, Ee Yuda, ni sawasawa na hesabu ya miji yako; na kama ilivyo hesabu ya njia za Yerusalemu, ndivyo mlivyosimamisha madhabahu za kitu kile cha aibu, madhabahu za kumfukizia Baali uvumba.
14Basi, usiwaombee watu hawa, wala usipaze sauti yako, wala kuwaombea dua watu hawa; maana sitawasikia wakati watakaponililia kwa ajili ya taabu yao.[#Kut 32:10; Yer 7:16]
15Mpenzi wangu afanya nini nyumbani mwangu, ikiwa amefanya uasherati? Je! Nadhiri zako na nyama takatifu zitakuondolea hatia? Ufanyapo maovu, ndipo uonapo furaha.[#Eze 16:25; Hag 2:12; Tit 1:15]
16BWANA alikuita jina lako, Mzeituni wenye majani mabichi, mzuri, wenye matunda mema; kwa kelele za mshindo mkuu amewasha moto juu yake, na matawi yake yamevunjika.
17Kwa maana BWANA wa majeshi, aliyekupanda, ametamka mabaya juu yako, kwa sababu ya maovu ya nyumba ya Israeli, na ya nyumba ya Yuda, waliyoyatenda juu ya nafsi zao wenyewe kwa kunikasirisha, wakimfukizia Baali uvumba.[#Zab 44:2; Isa 5:2]
18Tena BWANA akanijulisha haya, nami nikayajua; ndipo uliponionesha matendo yao.
19Lakini mimi nilikuwa kama mwana-kondoo mpole, achukuliwaye kwenda kuchinjwa; wala sikujua ya kuwa wamefanya mashauri kinyume changu, wakisema, Na tuuharibu mti pamoja na matunda yake, na tumkatilie mbali atoke katika nchi ya walio hai, ili jina lake lisikumbukwe tena.[#Zab 83:4]
20Lakini, Ee BWANA wa majeshi, uhukumuye haki, ujaribuye fikira na moyo, nijalie kuona kisasi chako juu yao; kwa maana nimekufunulia wewe neno langu.[#Zab 7:8,9; Mdo 17:31; 1 Sam 16:7; 1 Nya 28:9]
21Basi, kwa hiyo, BWANA asema hivi, juu ya watu wa Anathothi, watakao uhai wako, wakisema, Hutafanya unabii kwa jina la BWANA, usije ukafa kwa mkono wetu.[#Yer 1:1; Amo 2:12]
22Kwa sababu hiyo BWANA wa majeshi asema hivi, Tazama, nitawaadhibu watu hawa; vijana watakufa kwa upanga; wana wao na binti zao watakufa kwa njaa;
23wala hapatakuwa na mtu atakayesalia kwao; maana nitaleta mabaya juu ya watu wa Anathothi, mwaka wa kujiliwa kwao.[#Lk 19:44]