Mithali 21

Mithali 21

1Moyo wa mfalme huwa katika mkono wa BWANA;

Kama mifereji ya maji huugeuza popote apendapo.

2Kila njia ya mtu ni sawa machoni pake mwenyewe;[#1 Sam 16:7; Yer 17:10; Yn 2:24]

Bali BWANA huipima mioyo.

3Kutenda haki na hukumu[#Hos 6:6]

Humpendeza BWANA kuliko kutoa sadaka.

4Mwenye kiburi na moyo wa majivuno,[#Mit 24:20]

Taa yake ni dhambi.

5Mawazo ya wenye bidii huuelekea utajiri tu;

Bali kila mwenye pupa huuelekea uhitaji.

6Kupata akiba ya mali kwa ulimi wa uongo

Ni moshi upeperushwao; ni kutafuta mauti.

7Jeuri ya wabaya itawaondolea mbali;

Kwa sababu wamekataa kutenda hukumu.

8Njia yake aliyelemewa na dhambi imepotoka sana;

Bali mtu aliye safi, kazi yake ni sawasawa.

9Ni afadhali kukaa katika pembe ya darini,

Kuliko katika nyumba pana pamoja na mwanamke mgomvi.

10Nafsi ya mtu mbaya hutamani uovu;[#Yak 4:5]

Jirani yake hapati fadhili machoni pake.

11Mwenye mzaha aadhibiwapo, mjinga hupata hekima;

Na mwenye hekima afundishwapo, hupokea maarifa.

12Mwenye haki huitafakari nyumba ya mtu mbaya;[#1 Kor 10:10; Rum 2:8]

Jinsi wabaya waangushwavyo wakaangamia.

13Azibaye masikio yake asisikie kilio cha maskini,[#Zab 58:4; Zek 7:11; Mdo 7:57; Mt 7:2]

Yeye naye atalia, lakini hatasikiwa.

14Kipawa cha siri hutuliza hasira;

Na rushwa bindoni humliza ghadhabu kali.

15Ni furaha yao wenye haki kutenda hukumu;

Lakini ni uharibifu kwao watendao maovu.

16Mtu aikosaye njia ya busara

Atakaa katika mkutano wao waliokufa.

17Mtu apendaye anasa atakuwa maskini;

Apendaye mvinyo na mafuta hatakuwa tajiri.

18Mtu asiye haki ni fidia ya wenye haki;[#Isa 43:3,4]

Naye afanyaye hila ni badala ya watu wa adili.

19Ni afadhali kukaa katika nchi ya nyika;

Kuliko na mwanamke mgomvi, mchokozi.

20Kuna hazina ya thamani na mafuta katika maskani ya mwenye hekima;[#Zab 112:3; Mit 10:22; Mt 25:3]

Bali mwanadamu aliye mpumbavu huyameza.

21Aandamaye haki na fadhili,[#1 Kor 15:58]

Ataona uhai na haki na heshima.

22Mwenye hekima huupandia mji wao wenye nguvu;

Na kuziangusha nguvu za tumaini lao.

23Mtu azuiaye kinywa chake na ulimi wake,

Atajilinda nafsi yake na taabu.

24Mwenye kiburi na kutakabari, jina lake ni mbishi;

Hutenda mambo katika majivuno ya kiburi chake.

25Matakwa yake mtu mvivu humwua,

Kwa maana mikono yake hukataa kufanya kazi.

26Kuna atamaniye kwa choyo mchana kutwa;

Bali mwenye haki hutoa wala hanyimi.

27Sadaka ya wasio haki ni chukizo;

Si zaidi sana ailetapo mwenye nia mbaya!

28Shahidi wa uongo atapotea;

Bali mtu asikiaye atasema maneno yadumuyo.

29Asiye haki huufanya uso wake kuwa mgumu;

Bali mtu mnyofu huzifikiri njia zake.

30Hapana hekima, wala ufahamu,

Wala shauri, juu ya BWANA.

31Farasi huwekwa tayari kwa siku ya vita;

Lakini BWANA ndiye aletaye wokovu.

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya