Tito 1

Tito 1

1Salamu kutoka kwa Paulo, mtumwa wa Mungu na mtume aliyetumwa na Yesu Kristo. Kazi yangu ni kuwasaidia wateule wa Mungu kumwamini Yeye zaidi na kuyaelewa kwa kina mafundisho ya Kristo. Mafundisho haya yatawaongoza kuishi katika njia inayomtukuza na kumpendeza Mungu.

2Na kisha wakatarajie kuishi pamoja na Mungu milele. Kabla ya mwanzo wa ulimwengu, Mungu aliahidi uzima wa milele kwa watu wake.

3Na wakati sahihi ulipotimia aliidhihirisha ile habari njema. Ujumbe huo ulikabidhiwa kwangu kwa amri ya Mungu Mwokozi wetu kumwambia kila mtu.

4Nakuandikia wewe Tito, mwanangu halisi katika imani tunayoshiriki:

Neema na amani kutoka kwa Mungu Baba, na kutoka kwa Kristo Yesu Mwokozi wetu iwe nanyi.

Kazi ya Tito Krete

5Nilikuacha kule Krete ili uweze kuyakamilisha yale yaliyokuwa yamebaki kufanyiwa kazi. Kisha nakuagiza uteue wazee na kuwaweka kuwa viongozi katika kila mji.

6Anayeweza kuteuliwa ni yule ambaye halaumiwi kwa matendo yoyote mabaya, na aliye mwaminifu kwa mkewe, na anao watoto wanaoamini Mungu na ambao sio wakaidi.[#1:6 Kwa maana ya kawaida, “mtu mwenye mke mmoja”, yenye maana pia ameoa mara mmoja tu.; #1:6 Neno hli laweza kuwa na maana ya “waaminifu” au “waaminio”. Hapa, maana zote zaweza kujumuishwa. Linganisha kifungu hiki na 1 Tim 3:4.]

7Kwa sababu kila askofu, anao wajibu wa kuitunza kazi ya Mungu, anapaswa kuwa mtu asiyelaumiwa kwa kutenda mabaya yoyote. Asiwe mtu mkorofi. Asiwe mtu aliye mwepesi wa hasira. Asiwe mgomvi. Asiwe mtu mwenye kujipatia fedha toka kwa watu kwa njia ya udanganyifu.[#1:7 Hapa ina maana, “mwangalizi” ama “mzee”. Tazama katika Orodha ya Maneno.]

8Mzee anapaswa kuwa mtu anayewakaribisha watu nyumbani mwake. Anapaswa kuyapenda yaliyo mema. Azingatie kuishi maisha yaliyo matakatifu. Na awe na uwezo wa kudhibiti nafsi yake.

9Anapaswa kuwa mwaminifu kwa ujumbe ule ule wa kweli tunaofundisha. Kwa namna hiyo ataweza kuwatia moyo wengine kwa mafundisho ya kweli na yenye manufaa. Na ataweza kuwathibitishia wale wanaopinga mafundisho yake ya kuwa hawako sahihi.[#1:9 Kwa maana ya kawaida, “yaliyo sahihi”. Pia katika 2:1.]

10Aina hii ya mafundisho ni muhimu kwa sababu wako watu wengi wasiopenda kumsikiliza mtu yeyote. Hao wanazungumzia mambo yao wenyewe yasiyo ya maana na kuwapotosha wengine waiache kweli. Ninaongelea hasa baadhi ya Wayahudi waaminio.[#1:10 Kwa maana ya kawaida, “wale walio wa tohara”. Tazama Mdo 11:2; Gal 2:2.]

11Ni lazima wanyamazishwe kwani wanaivuruga jamii nzima kwa kufundisha mambo ambayo wasingepaswa kuyafundisha, lakini wanafanya hivyo ili kujipatia mapato yasiyo ya uaminifu!

12Mmoja miongoni mwa watu wa kwao, Nabii kutoka Krete, alisema:

“Wakrete ni waongo daima.

Si bora kuliko wanyama wa porini.

Daima wapo tayari kula,

lakini hawapendi kufanya kazi.”

13Usemi huu ni kweli, kwa hivyo wakaripie vikali ili wawe imara katika imani yao

14na wasiendelee kuzisikilliza simulizi zinazopotosha za Kiyahudi na amri za wanadamu walioiacha kweli.

15Kwa wale watu wenye mawazo yaliyo safi, kila kitu ni safi. Lakini hakuna kinachoweza kuwa safi kwa wasioamini ambao dhambi zao zimewafanya kuwa wachafu. Mawazo yao daima huwa yasiyo haki, na dhamiri zao pia zimekuwa chafu.

16Hao hudai kuwa wanamjua Mungu, lakini matendo yao maovu yanaonesha kwa hakika kuwa hawamjui. Ni watu wenye kuchukiza mno na wasiotii, na hawafai kwa lo lote lililo jema.

Agano Jipya: Tafsiri ya Kusoma-Kwa-Urahisi Toleo la Awali © 2017 Bible League International
Published by: Bible League International